Hamia kwenye habari

Kushoto: Ndugu na dada wakishiriki katika Maonyesho ya Kimataifa jijini Luanda, Angola. Kulia: Ndugu (katikati) akiwaonyesha wageni katika kibanda chetu jinsi funzo la Biblia linavyoongozwa

SEPTEMBA 12, 2024
ANGOLA

Zaidi ya Watu 200 Waonyeshwa Jinsi Funzo la Biblia Linavyoongozwa Kwenye Maonyesho ya Kimataifa ya Angola

Zaidi ya Watu 200 Waonyeshwa Jinsi Funzo la Biblia Linavyoongozwa Kwenye Maonyesho ya Kimataifa ya Angola

Maonyesho ya 39 ya Kimataifa ya Luanda yalifanyika Julai 23 hadi 28, 2024, jijini Luanda, Angola. Maonyesho hayo ya kila mwaka yalionyesha bidhaa mbalimbali kutoka makampuni 1,800 na yalihudhuriwa na karibu watu 100,000. Mashahidi wa Yehova walikuwa pia na kibanda chao na walionyesha machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha tisa. Kibanda hicho kilikuwa pia na sehemu ya kuketi ambapo wageni wangeweza kuonyeshwa jinsi funzo la Biblia linavyoongozwa. Mashahidi walionyesha jinsi funzo la Biblia linavyoongozwa mara 227 katika maonyesho hayo, na zaidi ya watu 100 waliomba watembelewe nyumbani kwao.

Mwanamke fulani alikuja kwenye kibanda hicho na akasema kwamba angependa kujifunza Biblia. Dada mmoja alijitolea kujifunza naye. Walipokuwa wakizungumza, mwanamke huyo aliuliza maswali mengi na alipendezwa sana na ahadi za Biblia za wakati ujao. Sasa anajifunza kwa ukawaida na dada huyo.

Dada akitumia kifaa cha kielektroni kuonyesha tovuti ya jw.org

Mwanamke mwingine alishangaa kujua kwamba tunafundisha watu Biblia bila malipo. Dada yetu alimweleza kwamba tunafanya hivyo kwa sababu tunataka kushiriki habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu na watu wengi iwezekanavyo.Dada yetu alipojua kwamba mwanamke huyo alikuwa amejifunza Biblia na Mashahidi hapo awali, alimwonyesha video Ni Nini Hutendeka Katika Jumba la Ufalme? Mwanamke huyo alifurahi kujua kwamba watu wote wanakaribishwa kuhudhuria mikutano, na akasema angependa kujua mengi zaidi.

Mwanamke kutoka Ureno alifurahi sana kuwaona Mashahidi wa Yehova kwenye maonyesho hayo. Alieleza kwamba mara nyingi yeye huzungumza na jirani yake ambaye ni Shahidi. Alisema hivi: “Ninavutiwa sana na tengenezo lenu, na ninataka kujua mengi kulihusu.” Mwanamke huyo aliahidi kwamba atakaporudi nyumbani atamwomba jirani yake amfundishe Biblia.

Tunafurahi kwamba watu wengi nchini Angola wanataka kujifunza mengi kuhusu Biblia na wanakubali kwa hamu mwaliko wa Yehova wa kuchukua “maji ya uzima bure.”​—Ufunuo 22:17.