Hamia kwenye habari

Wakimbizi katika kambi ya wakimbizi ya Lóvua wakihudhuria programu ya kusanyiko la mzunguko la Kiluba

SEPTEMBA 12, 2019
ANGOLA

Makusanyiko Yafanywa Katika Kambi ya Wakimbizi ya Angola Katika Kingala na Kiluba

Makusanyiko Yafanywa Katika Kambi ya Wakimbizi ya Angola Katika Kingala na Kiluba

Mei 25 na 26, 2019, programu ya kusanyiko la mzunguko yenye kichwa “Uwe Imara!” ilifanywa katika kambi ya wakimbizi ya Lóvua katika lugha ya Lingala na Tshiluba. Kambi hii iko umbali wa kilomita 1,022 kutoka mji mkuu wa Angola, Luanda. Wakati wa programu hiyo, kulikuwa na wahubiri 177 waliokuwa wakiishi katika kambi hiyo pamoja na familia zao. Hata hivyo, watu 380 walihudhuria programu ya lugha ya Lingala na watu 3 walibatizwa, na watu 630 walihudhuria programu ya lugha ya Kiluba na watu 6 walibatizwa.

Ndugu wengi waliokimbilia kwenye kambi ya Lóvua walifanya hivyo kwa sababu ya machafuko katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Ndugu zetu katika kambi ya Lóvua hawawezi kuhudhuria matukio ya kiroho katika miji mingine, kwa sababu ya vizuizi vya kusafiri kambini. Kwa hiyo, ofisi ya tawi ilipanga kuwe na makusanyiko ndani ya kambi na pia ikajenga Majumba mawili ya Ufalme ya muda. Majumba hayo ya Ufalme yanatumiwa na makutaniko manne—matatu ya Kiluba na moja la Kingala.

Mei 24, 2019, mwangalizi wa mzunguko pamoja na mwakilishi wa ofisi ya tawi walisafiri kwenda kwenye kambi ya Lóvua ili kusaidia kufunga mitambo ya sauti na kusimamisha jukwaa. Licha ya hali ngumu ambazo ndugu zetu wanakabili wakiwa wakimbizi, walichangia maturubai, nguzo, kamba, misumari, na vifaa vingine vilivyohitajika.

Baada ya programu, Honoré Lontongo, mtumishi wa huduma katika kutaniko moja la Kiluba katika kambi hiyo ya wakimbizi alisema hivi: “Kuona makusanyiko yakifanyiwa humu ndani ya kambi, licha ya hali ngumu, kunatufanya tuhisi upendo wa Yehova si kwetu tu tukiwa kikundi bali kwa ajili ya mtu mmojammoja. Nina furaha sana!”

Tutaendelea kusali kwa ajili ya ndugu zetu ambao walilazimika kuacha makao yao kwa sababu ya mchafuko wa kisiasa wa ulimwengu huu. Tunajua kwamba Yehova ataendelea kutuandalia chakula na utegemezo wa kiroho popote tulipo.—Waroma 8:38, 39.

 

Akina ndugu wakijenga jukwaa na kutayarisha vifaa vya sauti

Watu sita wanaotaka kubatizwa wakiwa wamesimama ili kujibu maswali ya ubatizo wakati wa kusanyiko la mzunguko la Kiluba

Ndugu na dada kutoka kusanyiko la Kingala wakitembea umbali wa kilomita mbili kutoka kwenye kambi ya wakimbizi ili kushuhudia ubatizo

Ndugu Johannes De Jager, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Angola, akiwa pamoja na ndugu na dada baada ya kusanyiko la Kingala