Hamia kwenye habari

MEI 28, 2021
AZERBAIJAN

Kamati ya Haki za Kibinadamu ya UN Yatetea Haki ya Mashahidi wa Yehova ya Kufanya Mikutano Yao ya Kidini

Kamati ya Haki za Kibinadamu ya UN Yatetea Haki ya Mashahidi wa Yehova ya Kufanya Mikutano Yao ya Kidini

Aprili 26, 2021, Kamati ya Haki za Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa ilitoa uamuzi muhimu katika kesi ya Aziz Aliyev and Others v. Azerbaijan. Huu ni uamuzi wa tatu wa Kamati hiyo unaowatetea Mashahidi wa Yehova nchini Azerbaijan na kukazia haki yetu ya kuabudu kwa amani.

Kesi hii inahusu uvamizi uliofanywa na polisi kinyume na haki katika jamii ya Aliabad iliyo katika Eneo la Zagatala. Septemba 21, 2013, polisi walivamia nyumba ya Ndugu Aziz Aliyev ambako Mashahidi wa Yehova kadhaa walikutanika ili kufanya mkutano wa kutaniko. Polisi hao walifanya msako katika nyumba hiyo na kuwatishia ndugu na dada, walichukua machapisho yao, stakabadhi zao za kisheria na za kitiba na pia pesa zao. Polisi hao waliwapeleka wote kituoni. Walipokuwa njiani, Dada Havva Aliyeva alipatwa na kifafa na kupoteza fahamu. Kwa sababu ya hilo polisi walilazimika kumpeleka hospitalini. Mara tu alipopata fahamu, alipelekwa kwenye kituo cha polisi ili kuhojiwa.

Baadaye, Mahakama ya Wilaya ya Zagatala iliamua kuwatoza ndugu na dada wengi kati yao faini ya Manat 1,500 za Azerbaijan (wakati huo zilikuwa dola 1,716 za Marekani). Mahakama ya Rufaa ya Sheki ilikubaliana na uamuzi huo usio wa haki wa mahakama ya wilaya. Baada ya ndugu na dada zetu kufanya yote wawezayo kukata rufaa nchini Azerbaijan, waliamua kukata rufaa kwenye Kamati ya Haki za Kibinadamu.

Kamati hiyo iliamua kwamba Azerbaijan ilikuwa imewatendea ndugu zetu kinyume na haki yao ya kuwa na uhuru wa kidini na haki yao dhidi ya kukamata na kuadhibiwa isivyo haki. Katika uamuzi wa Kamati hiyo, ilitajwa kwamba Mashahidi wa Yehova wanatendewa vibaya na wenye mamlaka na polisi ambao “waliwatishia kuwafunga gerezani, waliwatendea bila heshima na kudhihaki dini yao, lakini hawakuwaambia ikiwa kuna usumbufu wowote wanaofanya au ikiwa utendaji wao wa kidini na machapisho yao yana madhara yoyote.” Hivyo, nchi ya Azerbaijan iliambiwa iwafidie ndugu zetu na “kuchukua hatua zote zinazohitajika ili kuhakikisha kwamba hali kama hiyo isitokee tena wakati ujao, hilo linatia ndani kupitia sheria ya ndani ya nchi upya.”

Tunafurahi kwamba ndugu zetu nchini Azerbaijan waliruhusiwa kuabudu na kukutanika kwa uhuru katika miaka ya hivi karibuni. Tunamshukuru Mungu wetu, Yehova, kwamba ukweli unazidi kuthibitishwa kisheria katika mahakama za wakati wetu.—Wafilipi 1:7.