Hamia kwenye habari

FEBRUARI 4, 2022
AZERBAIJAN

Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Kibinadamu Imetetea Haki ya Akina Dada Waliokamatwa Nchini Azerbaijan Wakihubiri

Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Kibinadamu Imetetea Haki ya Akina Dada Waliokamatwa Nchini Azerbaijan Wakihubiri

Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Kibinadamu (CCPR) ilifanya maamuzi mawili mwezi Novemba na Desemba 2021 ambayo yalitetea haki ya Mashahidi wa Yehova kuwaeleza wengine kuhusu imani yao. Kesi zote mbili ziliwahusu akina dada ambao walikamatwa na wenye mamlaka nchini Azerbaijan kwa kuwaeleza wengine ujumbe wa Biblia.

Novemba 5, 2021, CCPR iliunga mkono kwamba Dada Matanat Gurbanova na Dada Saadat Muradhasilova wana haki ya kuhubiri. Dada hao walikamatwa mwezi Novemba 2014 baada ya wenye mamlaka kupokea malalamishi kutoka mtu asiyejulikana. Dada hao walitozwa faini ya Manat 1,500 za Azerbaijan (dola 880 za Marekani). CCPR ilifikia uamuzi kwamba ilikuwa kinyume cha sheria kuwakamata na ikaagiza kwamba Azerbaijan izuie jambo kama hilo lisitokee wakati ujao.

Matanat na Saadat, ambao ni dada wa tumbo moja, walisema hivi: “Ingawa maofisa wa polisi na hakimu walitaka kututisha, tukio hilo liliimarisha imani yetu. Kwa mara nyingine Yehova amethibitisha kwamba mkono wake si mfupi na kwamba anajua wakati wa kuwalinda watumishi wake na jinsi ya kufanya hivyo.”

Desemba 21, 2021, CCPR ilitoa uamuzi kama huo uliosema kwamba maofisa wa polisi nchini Azerbaijan walivunja sheria walipowakamata Dada Jeyran Azizova na Dada Gulnaz Israfilova kwa sababu ya “kuendeleza utendaji wa kidini nje ya eneo lao rasmi.” Katika uamuzi wake, CCPR ilithibitisha kwamba akina dada hao hawakukiuka sheria kwa kuwaeleza wengine kuhusu imani yao.

Novemba 2016, Jeyran na Gulnaz waliwaeleza wengine ujumbe wa Biblia walipokuwa wakiwatembelea marafiki wao katika Eneo la Goranboy, Azerbaijan. Ofisa mmoja wa eneo hilo alitoa malalamishi polisi, na akina dada hao wakakamatwa. Wakati wa kesi yao, hakimu aliwashtaki dada zetu kuwa wapelelezi na akawatoza faini ya Manat 2,000 za Azerbaijan (dola 1,176 za Marekani). Mahakama ya rufaa iliunga mkono uamuzi huo. Dada hao walikata rufaa kwenye CCPR.

Maamuzi ya kisheria yanayounga mkono haki zetu, yanatusaidia kuhubiri kwa uhuru, na hiyo ndiyo kazi muhimu zaidi. Tunashangilia pamoja na dada zetu walioweka mfano mzuri wa kuhubiri habari njema kwa ujasiri.—Mathayo 10:18.