Hamia kwenye habari

Katika mwaka wa 2019, Kimbunga Dorian kiliharibu Jumba pekee la Ufalme kwenye kisiwa cha Great Abaco, Bahamas. Jumba la Ufalme lililojengwa Upya lawekwa wakfu

JANUARI 26, 2023
BAHAMAS

Jumba la Ufalme Lililojengwa Upya Lawekwa Wakfu Bahamas

Jumba la Ufalme Lililojengwa Upya Lawekwa Wakfu Bahamas

Ndugu Mark Sanderson akitoa hotuba ya wakfu

Januari 7, 2023, Ndugu Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, aliweka wakfu Jumba la Ufalme lililojengwa upya kwenye kisiwa cha Great Abaco kilicho Bahamas. Jumba hilo la Ufalme lilikuwa limeharibiwa na Kimbunga Dorian, Septemba 2019. Janga la COVID-19 lilisimamisha kazi ya kurekebisha Jumba la Ufalme majuma matatu tu kabla ya tarehe ambayo kazi hiyo ilikuwa imepangiwa kukamilika, yaani, Machi 2020. Wajitoleaji wa ujenzi walirudi katika mwaka wa 2021 ili kukamilisha mradi huo.

Ndugu Sanderson alisema hivi katika hotuba yake yenye kusisimua: “Kimbunga hicho kilipopiga kisiwa hiki, kilibeba vitu vingi, lakini kwa hakika hakikubeba imani yenu. Na hakikubeba pia uhusiano wenu na Mungu.”

Jumba hilo lililojengwa upya sasa lina uwezo wa kustahimili kimbunga. Hilo ndilo Jumba pekee katika kisiwa hicho na linatumiwa na wahubiri 49 katika makutaniko mawili, moja la Kiingereza na lingine la Krioli ya Haiti. Programu hiyo ya wakfu ilihudhuriwa na watu 175 na kwenye mtandao vifaa 167 viliunganishwa. Wenyeji wa eneo hilo ambao ni Mashahidi na wale ambao si Mashahidi pia walialikwa kuhudhuria programu hiyo ya wakfu.

Ndugu Jake Majure alikuwa mmoja wa wajitoleaji wa ujenzi kazi ya kurekebisha iliposimamishwa. Alisema hivi: “Ilihuzunisha sana. Kazi ya kurekebisha nyumba za akina ndugu ilikuwa ikisonga kwa kasi, nalo Jumba la Ufalme lilikuwa karibu kukamilika ili liwe tayari kwa ajili ya Ukumbusho.” Alifaulu kurudi katika mwaka wa 2021 ili kusaidia katika kazi ya kukamilisha Jumba la Ufalme pamoja na marekebisho mengine ya nyumba za akina ndugu.

Programu ya kuweka Jumba la Ufalme wakfu ilikuwa tukio lenye shangwe

Ndugu Sanderson alisema: “Jumba hili la Ufalme ni uthibitisho wa kwamba watu wa Yehova wanafanya kazi kwa umoja na wanapendana. Nimefurahia pendeleo hili kubwa sana la kuwa hapa mwezi huu wa Januari 2023 na kuliona jengo hili lililokamilishwa na pia kuiona shangwe ya ndugu zetu.”

Tuna uhakika kwamba Jumba hili la Ufalme lililojengwa upya litamletea sifa Mungu wetu, Yehova.​—Ezra 3:10.