Hamia kwenye habari

Akina dada wakionyesha broshua Furahia Maisha Milele! huku gazeti Mnara wa Mlinzi lenye kichwa “Afya ya Akili—Msaada Kutoka Katika Biblia” likiangaziwa nyuma yao

SEPTEMBA 19, 2023
BOLIVIA

Elimu ya Afya ya Akili Yaangaziwa Kwenye Maonyesho ya Kimataifa ya Vitabu Nchini Bolivia

Elimu ya Afya ya Akili Yaangaziwa Kwenye Maonyesho ya Kimataifa ya Vitabu Nchini Bolivia

Maonyesho ya Kimataifa ya Vitabu ya Santa Cruz yalifanywa kuanzia Mei 31 hadi Juni 11, 2023 huko Santa Cruz de la Sierra, Bolivia. Zaidi ya wageni 120,000 walihudhuria maonyesho hayo. Kibanda kilichosimamiwa na ndugu zetu kilikazia gazeti Mnara wa Mlinzi Na. 1 2023, lenye kichwa “Afya ya Akili—Msaada Kutoka Katika Biblia.”

Toleo la Kihispania la gazeti Mnara wa Mlinzi Na. 1 2023 lenye kichwa “Afya ya Akili—Msaada Kutoka Katika Biblia”

Ndugu na dada 200 hivi walifanya kazi kwenye kibanda hicho wakati wa maonyesho hayo na walizungumza na wageni zaidi ya 20,000. Televisheni zilionyesha tovuti yetu, na wageni walijifunza jinsi ya kufanya utafiti kuhusu mada mbalimbali kwenye jw.org. Machapisho 5,500 yalitolewa na video 600 hivi zilionyeshwa. Isitoshe, watu 45 waliotembelea kibanda hicho waliomba funzo la Biblia kupitia fomu ya mtandaoni kwenye jw.org.

Baada ya mwanamke mmoja kuona kichwa kuhusu afya ya akili kwenye kibanda chetu, alizungumza na dada mmoja na kumweleza kwamba mama yake anapambana na matatizo ya afya ya akili na ya kihisia. Mwanamke huyo alitaja pia kwamba yeye binafsi anakabiliana na ugonjwa wa kuwa na wasiwasi kupita kiasi na kushuka moyo. Dada huyo alimsaidia mwanamke huyo kupakua gazeti Mnara wa Mlinzi linalohusu afya ya akili pamoja na broshua Furahia Maisha Milele! kwenye simu yake. Pia mwanamke huyo alijaza fomu ya mtandaoni ya jw.org kuomba funzo la Biblia mara moja.

Ndugu na dada kadhaa wakiwa ndani ya kibanda kwenye Maonyesho ya Kimataifa ya Vitabu

Mwanasaikolojia ambaye alipokea nakala ya gazeti Mnara wa Mlinzi kuhusu afya ya akili kwenye maonyesho hayo alisema hivi: “Ninapanga kushiriki makala hii na wagonjwa wangu. Habari hii na mistari ya Biblia iliyozungumziwa itawanufaisha.” Mwanamke mwingine ambaye mama yake alikufa hivi karibuni, alitiwa moyo sana baada ya kuonyeshwa makala yenye kichwa “Mzazi Anapokufa” iliyo chini ya sehemu yenye kichwa “Amani na Furaha” kwenye jw.org.

Kwa kuwa leo watu wengi sana wanakabiliana na matatizo ya afya ya akili na ya kihisia, ndugu na dada zetu nchini Bolivia walifurahi kuwasaidia watu kupata faraja kutokana na ushauri unaofaa ambao Yehova anatupa kupitia Neno lake, Biblia.​—Zaburi 34:18.