Hamia kwenye habari

OKTOBA 29, 2019
BRAZILI

Habari za Viziwi na Vipofu Kwenye Kibanda cha JW.ORG Katika Maonyesho ya Vitabu ya Kila Baada ya Miaka Miwili Huko Rio

Habari za Viziwi na Vipofu Kwenye Kibanda cha JW.ORG Katika Maonyesho ya Vitabu ya Kila Baada ya Miaka Miwili Huko Rio

Mashahidi wa Yehova walishiriki katika maonyesho ya 19 ya kimataifa ya vitabu yanayofanywa kila baada ya miaka miwili huko Rio de Janeiro. Yalifanyika katika ukumbi wa Riocentro Convention and Event Center kuanzia Agosti 30 hadi Septemba 8, 2019. Hayo ndiyo maonyesho makubwa zaidi ya kitamaduni nchini Brazili. Yalikuwa na vibanda 520, na yalivutia wageni 600,000 hivi. Ndugu zetu waliweka kibanda kilichotangaza tovuti yetu na jitihada zetu za kusambaza machapisho yanayotegemea Biblia. Katika siku kumi za maonyesho hayo ya vitabu, akina ndugu na dada 258 walijitolea kwenye kibanda hicho na kutoa machapisho 3,737.

Kibanda hicho kilikuwa na sehemu ya pekee kwa ajili ya wageni walio viziwi au walio na matatizo ya kusikia, na vipofu. Akina ndugu walionyesha video za Lugha ya Alama ya Brazili (LIBRAS), na wahubiri wanaojua vizuri lugha hiyo walikuwa tayari kuwasaidia wageni. Mmoja wa wajitoleaji alisema: “Watu walipofika kwenye kibanda hicho walijihisi huru kuzungumza nasi na hawakuona aibu. Muda wote kulikuwa na mjitoleaji aliyeeleza jinsi ya kutumia jw.org na mambo yanayotendeka kwenye funzo la Biblia.”

Mhubiri kipofu mwenye umri wa miaka kumi akimweleza mwanahabari jinsi ambavyo amenufaika na machapisho ya maandishi ya vipofu yaliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova

Kuna mwalimu ambaye alitembelea kibanda hicho akiwa na wanafunzi saba viziwi. Alifurahi kuona habari za lugha ya alama kwa ajili ya matineja kwenye jw.org. Alisema kwamba mara nyingi wazazi humwomba azungumze na watoto wao walio viziwi kuhusu mambo ya faragha. Mwalimu huyo alisema kwamba wakati ujao atawaelekeza wazazi hao kwenye tovuti yetu.

Dada akimwonyesha mgeni machapisho yanayotegemea Biblia

Vilevile kibanda hicho kilikuwa na maonyesho yaliyotafsiriwa katika lugha za asili ambazo zinapatikana kwenye jw.org, kama vile Guarani, Ticuna, na Xavante. Ricardo Carneiro, msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini humo anasema: “Tungependa kuwasaidia wenyeji wa asili waielewe Biblia vizuri zaidi katika lugha yao wenyewe”

Maonyesho ya Vitabu ya Kimataifa ya Rio huwatia moyo watu wasome ili waboreshe hali ya maisha nchini Brazili. Maelfu ya wageni waliotembelea kibanda cha jw.org walipewa fursa ya kusoma Biblia na machapisho mengine katika lugha yao, jambo ambalo limekuwa likiboresha maisha ya watu kwa karne nyingi.—2 Timotheo 3:16, 17.