Hamia kwenye habari

Kushoto: Ramani inayoonyesha jamii zilizotembelewa katika kampeni hiyo ya miezi minne. Picha ndogo (kushoto hadi kulia): Ndugu na dada wanaozungumza lugha za Wapishana-, Xavante-, na Hunsrik wakishiriki katika kazi ya kuhubiri

AGOSTI 8, 2024
BRAZILI

Kampeni ya Kuhubiri Nchini Brazili Yasaidia Kupanda Mbegu za Kweli ya Biblia Katika Lugha 11

Kampeni ya Kuhubiri Nchini Brazili Yasaidia Kupanda Mbegu za Kweli ya Biblia Katika Lugha 11

Kuanzia Machi 1 hadi Juni 30, 2024, zaidi ya Mashahidi 1,000 wa Yehova walishiriki katika kampeni kubwa ya kuhubiri kotekote nchini Brazili. Kampeni hiyo ilipangwa ifanyike wakati wa kutolewa kwa chapisho Furahia Maisha Milele! katika lugha 11 zinazozungumzwa nchini humo. Matokeo ni kwamba karibu watu 300 waliomba funzo la Biblia.

Dada wawili wakiongea na mwanamke anayezungumza Kihunsrik huko Nova Petrópolis

Wakati wa mazungumzo fulani, mwanamke mmoja huko Campinápolis anayezungumza lugha ya Xavante aliwauliza wahubiri hivi: “Ninyi ndio mnaotayarisha video za lugha yangu? Nimekuwa nikiwatafuta kwa muda mrefu. Sasa hatimaye nimewapata!” Alieleza kwamba hapo awali alijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova lakini akaacha kwa sababu hakuelewa Kireno. Hata hivyo, baada ya kufahamu kwamba machapisho na video zetu zinazotegemea Biblia sasa zinapatikana katika lugha ya Xavante, mwanamke huyo alianza kuwatafuta Mashahidi. Alianza tena kujifunza Biblia.

Huko Santa Maria de Jetibá, dada mmoja alizungumza mara tatu kwa muda mrefu na mwanamke aliyependezwa anayezungumza lugha ya Pomerania. Mara ya tatu dada yetu alipomtembelea, mwanamke huyo alisema kwamba alikuwa amesali siku moja kabla ya walipozungumza kwa mara ya kwanza, naye alimwomba Mungu amfundishe jinsi ya kumwabudu kwa njia inayofaa. Alikubali kwa hamu sana kujifunza Biblia.

Katika kijiji kimoja kidogo kusini mwa Brazili, ndugu zetu walikutana na mwanamke anayezungumza lugha ya Kaingang ambaye hakuwa anawafahamu kabisa Mashahidi wa Yehova. Ndugu zetu walimsomea Zaburi 83:18 na kumweleza kwamba Yehova ndilo jina la Mungu. Aliguswa moyo sana, naye akasema kwamba hakuna mtu aliyekuwa amemfundisha kwamba Mungu ana jina lake la kibinafsi. Alikubali kujifunza Biblia mara moja.

Furahia Maisha Milele! katika lugha ya Hunsrik, Kaingang, Kaiwá, Macushi, Nhengatu, Pomeranian, Sateré-Mawé, Talian, Ticuna, Wapishana, na Xavante. Kampeni hiyo ilipangwa ifanyike wakati ambapo chapisho hilo lilitolewa

Tunashangilia pamoja na ndugu na dada zetu nchini Brazili kwamba watu wengi sana wanajifunza mengi zaidi kuhusu “habari njema ya milele” zinazopatikana katika Neno la Mungu ili wajiunge nasi katika kumtukuza Yehova.​—Ufunuo 14:6, 7.