Hamia kwenye habari

Kituo kipya cha elimu ya Biblia huko Cabreúva, Brazili. Picha ndogo juu: Wanafunzi wakishiriki kipindi cha maswali na majibu

DESEMBA 20, 2023
BRAZILI

Kituo Kipya cha Elimu ya Biblia Chafunguliwa Nchini Brazili

Kituo Kipya cha Elimu ya Biblia Chafunguliwa Nchini Brazili

Desemba 3, 2023, Ndugu Eduardo Martines, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Brazili alitoa hotuba ya kuweka wakfu kituo kipya cha elimu ya Biblia huko Cabreúva, Brazili katika Jumba la Kusanyiko lililo karibu. Zaidi ya ndugu na dada 2,400 walihudhuria programu hiyo uso kwa uso, na wengine zaidi ya 4,900 waliunganishwa kupitia video mtandaoni.

Kushoto: Ndugu Eduardo Martines akitoa hotuba ya kuweka wakfu. Juu kulia: Wahudhuriaji wakifurahia programu. Chini kulia: Walimu waliofundisha shule hizo kwa muda mrefu wakihojiwa

Kituo hicho kipya cha elimu ya Biblia kitatumiwa hasa kwa ajili ya Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme na Shule ya Waangalizi wa Mzunguko na Wake Zao. Kituo hicho kinaweza kuwa na madarasa matatu kwa wakati mmoja hivyo jumla ya wanafunzi 600 hivi wataweza kuhudhuria shule kila mwaka.

Mwalimu akiongoza kipindi cha maswali na majibu

Mwaka wa 2020, ndugu zetu walinunua jengo la hoteli na kuligeuza pole kwa pole ili kulifanya kituo cha elimu ya Biblia. Wajitoleaji waliendelea na kazi hiyo katika kipindi cha COVID-19 huku wakichukua tahadhari. Walitokeza madarasa 3, vyumba 54 vya makazi, chumba cha kulia chakula, na ofisi kadhaa. Mara tu baada ya kukamilisha ujenzi huo, mipango ilifanywa ili kuwa na siku ya wageni. Kusudi kuu lilikuwa kuwasaidia watu katika eneo hilo, kutia ndani wenye mamlaka, kuwafahamu Mashahidi wa Yehova na pia kazi tunayofanya ya kuwafundisha watu Biblia. Mtu mmoja mwenye mamlaka aliyetembelea majengo hayo alisema: “Kazi ambayo imefanywa hapa ni maridadi na ya kiwango cha juu sana. Tunapofanya kitu kwa ajili ya Mungu, kinapaswa kuwa hivi.”

Kushoto: Mapokezi ya kituo hicho kipya cha elimu. Kulia: Makazi ya wanafunzi

Ndugu Rogério Braganholo, aliyeshiriki katika kazi ya ukarabati, alisema hivi: “Tuliona wazi mwongozo wa Yehova muda wote wa mradi huu. Kumwona akibariki jitihada zetu kulikazia ukweli wa maneno ya Zaburi 127:1: ‘Yehova asipoijenga nyumba, wale wanaoijenga wanafanya kazi ngumu ya bure.’”

Tunafurahi sana kwamba kituo hicho kipya cha elimu ya Biblia kimefunguliwa na kwamba kitawasaidia ndugu na dada wengi zaidi nchini Brazili kuboresha “ustadi [wao] wa kufundisha.”​—Tito 1:9.