Hamia kwenye habari

JUNI 25, 2020
BRAZILI

Kuwaandalia Msaada Ndugu Zetu Walio Amazoni

Kuwaandalia Msaada Ndugu Zetu Walio Amazoni

Halmashauri ya Tawi ya Brazili imeunda Halmashauri 18 za Kutoa Msaada ili kuwasaidia wahubiri wanaopambana na hali mbaya ya kiuchumi iliyosababishwa na ugonjwa wa virusi vya corona. Halmashauri hizo zinasaidia makutaniko 12,000 nchini kote, kutia ndani ndugu zetu wanaoishi mbali katika eneo la Mto Amazoni. Kufikia sasa, familia 131 zinazoishi huko Amazoni zimepokea msaada huo.

Halmashauri za Kutoa Msaada zilizo katika jiji la Manaus, mji mkuu wa jimbo la Amazonas, zilitayarisha vifurushi vilivyo na mahitaji ya msingi ya kutosha mwezi mmoja. Ndani ya vifurushi hivyo, kulikuwa na maharagwe, unga wa muhogo, mchele, maziwa ya unga na pia vitu vingine kama sabuni, karatasi za choo, miswaki na dawa ya meno. Ndugu hao walisafirisha mizigo hiyo kupitia bandari ya Manacapuru, kisha wakaisambaza kwa mashua hadi maeneo ya mbali kama vile Membeca na Lago do Castanho.

Dada Marinelma anayeishi katika eneo la Lago do Castanho, alisema hivi baada ya kupokea kifurushi hicho: “Kwanza, ninamshukuru Yehova kwa kututunza. Tulikuwa na uhitaji mkubwa kwa kuwa hatukuwa na uwezo wa kununua chakula. Pia, ningependa kuwashukuru ndugu na dada kwa ukarimu wao na upendo. Mwanangu mwenye umri wa miaka sita aliniona nikifungua mzigo huo na kupanga vitu, kwa hiyo, nikatumia fursa hiyo kumweleza jinsi Yehova alivyowaongoza akina ndugu kutusaidia. Kisha akasema, ‘Mama, tunaweza kusali na kumshukuru Yehova?’”

Ndugu Jonas Monteiro anayeishi na familia yake katika jiji la Caapiranga, aliiandikia barua Halmashauri ya Kutoa Msaada, iliyosema hivi: “Asanteni sana kwa msaada mliotupa. Tumeona upendo wa Yehova kupitia kwenu. Ni pendeleo kubwa sana kuwa sehemu ya familia hii ya ulimwenguni pote.”

Ndugu walio katika Halmashauri za Kutoa Msaada wametiwa moyo pia. Isaac Emannuel Ramalho de Oliveira, mzee anayetumikia katika halmashauri moja, alisema hivi: “Kila siku ambayo ninafanya kazi katika Halmashauri ya Kutoa Msaada, ninahisi imani yangu ikiimarishwa sana. Nina uhakika kwamba kazi hii itanisaidia mimi zaidi kuliko inavyowasaidia wengine.”

Imani yetu inaimarishwa kuona jinsi Yehova anavyowatunza watumishi wake popote walipo wakati wa ugonjwa huu.—Zaburi 94:14.