Hamia kwenye habari

Kushoto: Ndugu Nathan Knorr atembelea ofisi ya tawi jijini Rio de Janeiro Aprili 1949. Kulia: Ndugu Knorr akitoa hotuba kwenye kusanyiko jijini São Paulo lililofanyika Aprili 9-10, 1949

JUNI 22, 2022
BRAZILI

Miaka Sabini na Tano ya Kutambuliwa Kisheria Nchini Brazili

“Imani Yetu, Shauku Yetu, na Uhakika Wetu Katika Yehova Haujawahi Kuyumba”

Miaka Sabini na Tano ya Kutambuliwa Kisheria Nchini Brazili

Juni 23, 1947, Mashahidi wa Yehova walisajili shirika la Sociedade Torre de Vigia de Bíblias e Tratados (Watch Tower Bible and Tract Society) nchini Brazili. Shirika hilo la kisheria limetumiwa nchini Brazili kwa miaka 75 sasa. Ndugu zetu walivumilia upinzani kwa miaka mingi kabla ya kutambuliwa kisheria.

Oktoba 13, 1945, wahubiri nchini Brazili waliandika barua ya malalamiko na kuwaomba watu waliokubaliana na malalamiko yao watie sahihi ili kuunga mkono jitihada zao za kutaka kutambuliwa kisheria. Kote kote nchini wahubiri 400 hivi walipata sahihi 44,411. Kisha walituma barua hiyo ikulu lakini hawakupata majibu yoyote.

Mwaka wa 1946, Brazili ilipata katiba mpya. Katiba hiyo ilikuwa na sheria ambazo ziliruhusu shirika la Watch Tower Bible and Tract Society kusajiliwa. Mwaka huo kulikuwa na wastani wa wahubiri 442 waliokuwa wakihubiri kila mwezi.

Viongozi wa kidini hawakufurahi Mashahidi walipotambuliwa kisheria. Miaka mitatu baadaye, Novemba 3, 1949, rais wa Brazili alishinikizwa na viongozi wa kidini kutia sahihi sheria ya kusimamisha utendaji wa shirika la Watch Tower Society na kulifunga. Akina ndugu walipinga uamuzi huo mahakamani. Kesi hiyo iliendelea hadi Aprili 8, 1957, rais mpya wa nchi hiyo alipofanya uamuzi uliounga mkono shirika la Watch Tower Bible and Tract Society.

Ingawa akina ndugu walikabiliana na matatizo ya kisheria, Yehova aliendelea kubariki kazi ya kuhubiri. Ndugu Djalma Mendes Souto, aliyebatizwa mwaka wa 1941 alikuwa mojawapo wa washirika wa kwanza wa Watch Tower Society nchini Brazili, alisema hivi: “Imani yetu, shauku yetu, na uhakika wetu katika Yehova haujawahi kuyumba, na kwa sababu hiyo, idadi ya wahubiri inaendelea kuongezeka. Katika mwaka wa 1947, tulifurahi sana kwa sababu kwa mara ya kwanza tulikuwa na wahubiri zaidi ya 1,000.”

Tangu wakati huo, idadi ya Mashahidi wa Yehova nchini Brazili imeongezeka kwa kasi. Katika mwaka wa 2021, Brazili ilifikia kilele kipya cha wahubiri 913,479, na watu 2,184,856 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kusanyiko la 2021 “Uwe Mwenye Nguvu kwa Imani!” lilitafsiriwa katika lugha 15, kutia ndani lugha 10 za asili.

Tunatiwa moyo sana na jinsi Yehova anavyobariki kazi ya kuhubiri nchini Brazili. Uvumilivu wa ndugu zetu licha ya matatizo ya kisheria unatuthibitishia kwamba Yehova huwaokoa wale wanaomtumaini.​—Isaya 25:9.