Hamia kwenye habari

Kushoto: Ofisi ya tawi ya Brazili iliyoko nje ya jiji la São Paulo. Kulia: Wajitoleaji wanaofanya kazi ya kukarabati ofisi ya tawi ya Brazili

MEI 6, 2022
BRAZILI

Ukarabati wa Ofisi ya Tawi ya Brazili Umeanza

Ukarabati wa Ofisi ya Tawi ya Brazili Umeanza

Mradi mkubwa wa ukarabati wa ofisi ya tawi ya Brazili umeanza. Ofisi hiyo ipo umbali wa kilomita 140 upande wa magharibi wa jiji la São Paulo. Kusudi la kufanya ukarabati huo ni kuboresha majengo ya Betheli na kubadilisha vifaa vilivyotumiwa katika ujenzi wa awali na kuboresha mwonekano wa majengo hayo. Ukarabati wa majengo ya Betheli hutokeza changamoto kadhaa. Ukarabati huo unapaswa kupangwa katika njia ambayo hautaathiri kazi nyingine zinazofanywa Betheli. Kwa mfano, Wanabetheli wanapaswa kukaa kwenye vyumba vingine kwa muda wakati vyumba vyao vinakarabatiwa. Inakadiriwa kwamba mradi huo utakamilika ndani ya miaka mitano.

Akina ndugu watafanya ukarabati huo kwenye eneo lenye ukubwa wa mita za mraba 75,000 hivi, ambalo linatia ndani ofisi zote na vyumba 650 vya makazi. Mabadiliko hayo yatafanya majengo ya Betheli yatumiwe vizuri zaidi na pia yatakuwa yanaweza kubadilishwa kulingana na uhitaji uliopo. Kwa mfano, ofisi zitakuwa na kuta zinazoweza kuhamishwa ili kubadili jengo liendane na uhitaji. Eneo dogo litakalotumiwa kwa ajili ya kupikia litaongezwa kwenye kila chumba, na pia eneo la kufulia nguo litapanuliwa zaidi. Vifaa vipya ambavyo ni bora zaidi kwa mazingira vitawekwa ili kupunguza kiasi cha maji na umeme kinachotumiwa.

Ndugu na dada ambao wanajitolea kufanya kazi kwenye mradi wataishi kwa muda ndani ya eneo la ofisi ya tawi. Kwa mfano, jengo la kuhifadhia vitu limegawanywa na kuwa vyumba 25 kwa ajili ya wajitoleaji. Kwa kuongezea, makontena 91 yamegeuzwa na kuwa makazi ya muda yaliyo kwenye shamba la Betheli linalopakana na ofisi ya tawi.

Makontena yanayotumiwa yakiwa makazi ya muda kwa ajili ya wajitoleaji

Ndugu Joel Grigor, mjenzi anayefanya kazi kwenye mradi huo, anasema hivi: “Tumejionea jinsi tengenezo la Yehova linavyotekeleza mradi huu na pia kuwazoeza watu wake. Wengi wa wajitoleaji hao walifika kwenye mradi bila ujuzi wowote au wakiwa na ujuzi mdogo tu, lakini sasa wamezoezwa vizuri hivi kwamba wanawazoeza wengine.”

Tuna uhakika kwamba Yehova ataendelea kuwabariki watu wake ‘wanapojitoa kwa hiari’ katika mradi huu na miradi mingine ya kitheokrasi.​—Zaburi 110:3.