Hamia kwenye habari

Ndugu Tesfazion Gebremichael amekuwa gerezani kwa miaka 11 nchini Eritrea

OKTOBA 26, 2022
ERITREA

Tume ya Uhuru wa Ibada wa Kimataifa ya Marekani Imeagiza Ndugu Mwenye Umri wa Miaka 80 Aachiliwe Huru Nchini Eritrea

Tume ya Uhuru wa Ibada wa Kimataifa ya Marekani Imeagiza Ndugu Mwenye Umri wa Miaka 80 Aachiliwe Huru Nchini Eritrea

Tume ya Uhuru wa Ibada wa Kimataifa ya Marekani (USCIRF) imeeleza wasiwasi wake kuhusu Ndugu Tesfazion Gebremichael ambaye amekuwa gerezani nchini Eritrea kwa zaidi ya miaka 11. Tovuti ya USCIRF imesema hivi: “Umri wa Gebremichael unazidi kusonga—sasa ana umri unaozidi miaka 80—umri ambao hauwezi kustahimili maisha ya gerezani kwa sababu ya afya.” Oktoba 7, 2022, Kamishna mmoja wa tume hiyo anayeitwa Frederick Davie alisema hadharani kwamba Ndugu Gebremichael anapaswa kuachiliwa huru.

Julai 20, 2011, wenye mamlaka walimkamata Ndugu Gebremichael alipokuwa akizungumza na wengine kuhusu imani yake. Ingawa amezaliwa nchini Eritrea, Ndugu Gebremichael si raia wa nchi hiyo kwa sababu serikali ya Eritrea iliwanyang’anya Mashahidi wote wa Yehova uraia wao mwaka wa 1994.

Ndugu Gebremichael alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova Januari 1971. Katika jamii, anajulikana kama mtu mwenye upendo, fadhili, na baba mzuri anayejali familia yake na anayependa kuwasaidia wengine. Mwaka wa 1974, alifunga ndoa na Lemlem, ambaye pia ni Shahidi wa Yehova. Wenzi hao wana watoto wanne na wajukuu watano.

Dada Gebremichael anasema hivi: “Ingawa nina wasiwasi kuhusu afya ya mume wangu huko gerezani, na ninakosa sana upendo na utegemezo wake, ninajua Yehova atamtunza. Ninavutiwa na ushikamanifu wa mume wangu na jinsi alivyoazimia kudumisha utimilifu wake. Kila ninapotafakari andiko la Mhubiri 10:4 linanitia moyo kuendelea kuwa mtulivu licha ya changamoto ambazo familia yetu inakabili.”

Tangu mwaka wa 1991, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakiteswa sana nchini Eritrea. Ingawa kati ya Desemba 2020 na Februari 2021, Mashahidi 32 waliachiliwa kutoka gerezani chini ya masharti fulani, bado ndugu na dada zetu 20 wamebaki gerezani. Ndugu na dada hao wamefungwa vifungo visivyo na mwisho, yaani, hawajapewa tarehe hususa ambayo vifungo vyao vitaisha. Kwa kuwa haiwezekani kufanya mipango yoyote ya kujitetea kisheria ni kana kwamba wamepewa kifungo cha maisha.

Mashiriki makubwa ya kimataifa ya kutetea haki za kibinadamu yamekemea tena na tena ukiukaji huo wa haki za msingi za kibinadamu unaoendelea nchini Eritrea na pia mashirika hayo yamehimiza nchi hiyo ishughulikie suala hilo. Katika mwaka wa 2016, Tume ya Umoja wa Mataifa ya Kuchunguza Haki za Kibinadamu Nchini Eritrea ilitangaza kwamba wenye mamlaka nchini Eritrea wametenda “uhalifu dhidi ya binadamu” kwa kuwatesa Mashahidi wa Yehova na watu wengine pia.

Sera ya kikatili ya nchi hiyo inaonekana wazi kupitia mfano wa Ndugu Gebremichael, kwa kuwa anaendelea kubaki gerezani licha ya kwamba ana umri mkubwa. Tangu 2011, Mashahidi wanne wamekufa gerezani na Mashahidi wengine watatu wenye umri mkubwa walikufa muda mfupi baada ya kuachiliwa huru kwa sababu ya hali mbaya walizokabili walipokuwa gerezani.

Wenye mamlaka nchini Eritrea wamekataa maombi ya Mashahidi wa Yehova ya kujadili suala hilo.

Tunasali kwa ajili ya ndugu na dada zetu ambao wanaendelea kubaki gerezani. Tuna uhakika kwamba Yehova ataendelea kuwategemeza.​—Waebrania 13:3.