Hamia kwenye habari

ERITREA

Maelezo Mafupi Kuhusu Eritrea

Maelezo Mafupi Kuhusu Eritrea

Mashahidi wa Yehova wanakabili mateso makali nchini Eritrea. Serikali ya Eritrea imeendelea kuwafunga, kuwatesa, na kuwasumbua Mashahidi wa Yehova tangu nchi hiyo ilipopata uhuru mwaka 1993. Rais alitoa amri Oktoba 25, 1994, iliyotangaza kwamba Mashahidi “wamefuta uraia wao nchini Eritrea” kwa kukataa kushiriki katika shughuli za kisiasa na kutojiunga na jeshi. Kwa hiyo, serikali inawanyima Mashahidi haki zao za msingi za kiraia.

Kwa sababu ya mateso na hali ngumu zinazoendelea kwa miaka mingi, Mashahidi wengi wameamua kuikimbia nchi hiyo. Waliobaki wanaendelea kutendewa isivyo haki na wanafanya shughuli za dini kwa tahadhari kubwa. Serikali ya Eritrea imewakamata na kuwafunga Mashahidi kwa miaka mingi. Wengine wamefungwa kwa kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri, wengine kwa sababu ya kuhudhuria mikutano ya dini au kuzungumza na watu wengine kuhusu ujumbe wa Biblia, na wengine wamefungwa kwa sababu zisizoeleweka. Wafungwa hao wanatia ndani wanaume na wanawake wenye umri mkubwa na wakati mwingine hata watoto. Wanaume watatu ambao ni Mashahidi wanaendelea kutumikia kifungo kwa zaidi ya miaka 20. Wamepelekwa gerezani bila kufunguliwa mashtaka au kuhukumiwa.

Mataifa mengine yameangazia mateso wanayokabili Mashahidi wa Yehova nchini Eritrea. Maofisa wa serikali kutoka Afrika, Ulaya, na Marekani wamejadili jambo hilo na maofisa wa Eritrea lakini serikali haijachukua hatua yoyote. Pia, Mashahidi wamepeleka maombi mengi ya kukutana na maofisa wa serikali waliopo jijini Asmara ili kutatua tatizo hilo, lakini serikali imekataa.