Hamia kwenye habari

OKTOBA 19, 2016
ERITREA

Mateso ya Mashahidi wa Yehova Nchini Eritrea Yakaziwa Uangalifu wa Pekee Kimataifa

Mateso ya Mashahidi wa Yehova Nchini Eritrea Yakaziwa Uangalifu wa Pekee Kimataifa

Mashahidi wa Yehova wananyanyaswa zaidi nchini Eritrea kuliko nchi nyingine duniani. Tangu nchi hiyo ilipopata uhuru mwaka wa 1993, Mashahidi wamefungwa, kuteswa, na kutengwa. Wanateswa kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa na kukataa kuchukua silaha dhidi ya wanadamu wenzao.

Kwa sasa, Mashahidi 54 wa Yehova wamefungwa gerezani nchini Eritrea. Kwa miaka 22 iliyopita, Mashahidi hao wote kasoro mmoja tu wamefungwa bila mashtaka maalumu wala kesi zao kusikilizwa. Watatu wamekuwa gerezani tangu mwaka wa 1994 kwa kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri.

Hangaiko la Jumuiya ya Kimataifa Laongezeka

Tangu mateso yalipoanza, mashirika ya haki za kibinadamu pamoja na mashirika ya serikali yameshutumu vitendo vya kuteswa ambavyo Mashahidi wa Yehova wanafanyiwa nchini Eritrea. Hata hivyo, hivi karibuni, Tume ya Uchunguzi ya Haki za Kibinadamu nchini Eritrea (COIE), ambayo imepewa mamlaka na Umoja wa Mataifa, imetoa taarifa nyingi za kimataifa kuhusu hali mbaya ambayo Mashahidi wanakabili. Katika ripoti iliyotolewa na tume hiyo kwenye Baraza la Umoja wa Mataifa la Haki za Kibinadamu (HRC) mnamo Juni 2015, COIE ilitia ndani sehemu yenye habari kuhusu jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyotendewa vibaya na kubaguliwa.

Juni 21, 2016, COIE ilipeleka ripoti yake ya pili iliyokuwa na habari zaidi kwa HRC. COIE ilihimiza Eritrea “iheshimu uhuru wa dini au imani” na “ikomeshe vifungo visivyozingatia haki na kuwaweka watu mahabusu kwa sababu ya imani yao ya kidini, hasa wafuasi wa dini fulani, kama vile Mashahidi wa Yehova, . . . na iwaachilie huru mara moja na bila masharti wote waliofungwa kinyume cha sheria na bila kuzingatia haki.”

Katika ripoti hiyo, COIE ilifikia mkataa kwamba matendo yanayofanywa nchini Eritrea ya “kuwatesa watu kwa misingi ya kidini na ya kikabila” ni kinyume na sheria za kimataifa na ni “uhalifu dhidi ya binadamu.” Jumuiya ya kimataifa inaona mateso hayo kuwa mojawapo ya ukiukaji mbaya zaidi wa haki za kibinadamu. Oktoba 27, 2016 COIE itawasilisha ripoti ya karibuni kwenye Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Je, Eritrea Itaacha Kuwatendea Isivyo Haki Mashahidi?

Mashahidi wa Yehova duniani pote wanahangaishwa sana na hali zinazowapata waabudu wenzao nchini Eritrea. Wanaisihi sana serikali ya Eritrea iache kuwatesa Wakristo hao waaminifu na kuwaruhusu wafurahie haki zao za msingi na ambazo pia ni za lazima.