Hamia kwenye habari

APRILI 26, 2017
FILIPINO

Mashahidi Wapanga Kazi ya Kujenga Upya Baada ya Kimbunga Nock-Ten

Mashahidi Wapanga Kazi ya Kujenga Upya Baada ya Kimbunga Nock-Ten

MANILA, Filipino—Mashahidi wa Yehova nchini Filipino wameanzisha mradi wa kutoa msaada kwa ajili ya kurekebisha na kujenga upya nyumba zilizoharibiwa na Kimbunga Nock-Ten (wenyeji walikiita “Nina”).

Jason Dotimas (kushoto) na Bethel Alvarez (kulia), wajitoleaji Mashahidi wa ujenzi, wakijenga upya Jumba la Ufalme lililo kwenye mji wa Polangui, Filipino. Wote walisafiri kilomita zaidi ya 650 ili kusaidia kazi ya kutoa msaada.

Katika Desemba 25, 2016, Nock-Ten, kimbunga kibaya sana, kilikumba eneo la Bicol, na kusababisha uharibifu mkubwa. Kulingana na ripoti fulani, dhoruba hiyo iliwaua watu 10 na kuharibu majengo zaidi ya 390,000. Ingawa hakuna Shahidi wa Yehova aliyekufa au kuumia sana, nyumba zaidi ya 300 za Mashahidi na majengo wanayofanyia ibada 24 (yanaitwa Majumba ya Ufalme) yaliharibiwa. Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Filipino walianzisha kamati ya kutoa msaada iliyofanya kazi katika jiji la Naga City ili kuwasaidia Mashahidi walioathiriwa.

Dean Jacek, msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Filipino alisema hivi: “Kufikia sasa, wajitoleaji wamerekebisha nyumba 271 na Majumba ya Ufalme 22. Vikosi vyetu vya kutoa msaada wa ujenzi vitaendelea kufanyia kazi nyumba 38 zilizosalia na Majumba ya Ufalme 2. Tuna lengo la kukamilisha kazi hiyo kufikia mwishoni mwa Aprili 2017.”

Nyumba zilizokamilishwa. Wakitumia mbinu ya kukusanya na kutengeneza mapema sehemu mbalimbali za nyumba, nyumba inaweza kujengwa kwa siku sita.

Kazi ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova, kutia ndani kutoa msaada, inasimamiwa na Baraza Linaloongoza na kutegemezwa na michango ya hiari. Kati ya Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni 8 ulimwenguni pote, 209,000 wanaishi nchini Filipino.

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

David A. Semonian, Ofisi ya Habari za Umma, +1-845-524-3000

Filipino: Dean Jacek, +63-2-224-4444