Hamia kwenye habari

Juu kushoto: Mwakilishi kutoka ofisi ya tawi ya Ghana akizungumza kwenye eneo la maonyesho. Chini kushoto: Nje ya Jumba la Makumbusho ya Kitaifa, jijini Accra, Ghana. Kulia: Picha mbalimbali wakati wa maonyesho hayo ya pekee

JUNI 19, 2024
GHANA

Kazi ya Utafsiri ya Mashahidi wa Yehova Yaonyeshwa Kwenye Jumba la Makumbusho ya Kitaifa la Ghana

Kazi ya Utafsiri ya Mashahidi wa Yehova Yaonyeshwa Kwenye Jumba la Makumbusho ya Kitaifa la Ghana

Kuanzia Aprili 11 hadi Juni 11, 2024, Jumba la Makumbusho ya Kitaifa la Ghana lililoko jijini Accra, Ghana, lilikuwa na maonyesho yenye kichwa “Kutolewa kwa Machapisho na Elimu ya Biblia Katika Lugha za Asili Nchini Ghana.” Zaidi ya watu 1,300 walitembelea maonyesho hayo.

Mwaka wa 1937, Mashahidi wa Yehova walianza kutafsiri machapisho ya Biblia nchini Ghana, ambayo hapo awali ilijulikana kama Gold Coast. Leo, ofisi ya tawi ya Ghana inatafsiri machapisho katika lugha 12 zinazozungumzwa nchini Ghana. Maonyesho hayo yalitia ndani video, machapisho, na mambo mengine yanayoonyesha historia hiyo ndefu. Pia, maonyesho hayo watu walionyeshwa jinsi ilivyo rahisi kupata na kutumia machapisho yaliyotafsiriwa kwenye jw.org.

Jumba la Makumbusho ya Kitaifa nchini Ghana pamoja na timu ya maprofesa wanne kutoka chuo kikuu cha Ghana, walishirikiana na ofisi ya tawi kutayarisha maonyesho hayo. Wakiwa na lengo la kuboresha kazi ya uchapishaji na utafsiri inayofanywa na serikali nchini Ghana, maprofesa hao walijifunza kuhusu mbinu ambazo Mashahidi wa Yehova wanatumia katika kazi ya utafsiri. Utafiti huo ulitia ndani ziara ya profesa Dakt. Araba Osei-Tutu, ambaye alitembelea Makao Makuu ya Mashahidi wa Yehova yaliyoko Warwick, New York, Marekani. Isitoshe, timu hiyo ya maprofesa ilitembelea ofisi ya tawi ya Ghana.

Kushoto: Dakt. Araba Osei-Tutu akizungumza wakati wa sherehe ya ufunguzi wa maonyesho hayo. Kulia: Machapisho ya lugha mbalimbali zinazozungumzwa nchini Ghana

Katika hotuba yake wakati wa kuanzishwa kwa maonyesho hayo, Dakt. Osei-Tutu alisema hivi: “Mashahidi wa Yehova wamefanya kazi kubwa sana ya kuwasaidia watu kujifunza kusoma na kuandika, hasa katika lugha zetu za asili. . . . Tunatumia fursa hii . . . kumshukuru kila mmoja ambaye ameshiriki katika kazi hiyo.”

Baada ya kutembelea maonyesho hayo, Profesa Yaw Sekyi-Baidoo wa Chuo Kikuu cha Elimu cha Winneba alisema hivi: “Sikuzote nimewaona Mashahidi wa Yehova kuwa wafundishaji, lakini nimestaajabishwa sana kuona upana wa kazi yao ya utafsiri.”

Maprofesa wa Chuo Kikuu cha Ghana, wafanyakazi wa Jumba la Makumbusho ya Kitaifa nchini Ghana, na wasomi wengine, wakipiga picha pamoja na baadhi ya ndugu na dada waliosaidia katika maonyesho hayo

Msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Ghana alisema hivi: “Inatia moyo sana kuona watu wa Yehova wakithaminiwa kwa sababu ya kazi ya kuwaelimisha watu katika jamii zao. Ni wazi kwamba Yehova anabariki jitihada za kuwasaidia watu wa namna zote wamjue.”​—Yohana 17:3.