Hamia kwenye habari

MEI 15, 2017
HAITI

Jitihada za Kutoa Msaada Baada ya Tufani Matthew Zinakaribia Kukamilika Nchini Haiti

Jitihada za Kutoa Msaada Baada ya Tufani Matthew Zinakaribia Kukamilika Nchini Haiti

Kamati ya kutoa msaada ilibadili paa katika nyumba hii.

PORT-AU-PRINCE, Haiti—Tufani Matthew, ilikadiriwa kuwa dhoruba kali zaidi kukumba Haiti kwa zaidi ya miaka 50. Tufani hiyo ilikumba taifa hilo Oktoba 4, 2016, na kusababisha uharibifu kama ulioonekana baada ya tetemeko la mwaka wa 2010. Kama ilivyoripotiwa katika Tovuti yetu jw.org Habari katika Oktoba 24, 2016, mwanzoni Mashahidi wa Yehova waliandaa chakula, dawa, na mahema. Baada ya kukagua kikamili uharibifu uliotokea, katika Januari 1, 2017, Mashahidi walianzisha awamu ya pili ya kutoa msaada, ambayo ilitia ndani kutumia kamati tatu za kutoa msaada kusimamia vikosi 14 vya ujenzi ambavyo vilianza kazi ya kurekebisha nyumba 203 zilizoharibiwa. Mashahidi wanatarajia kumaliza kazi hiyo ya kutoa msaada mwezi Juni 2017.

Daniel Lainé, msemaji wa ofisi ya Mashahidi ya Port-au-Prince, anasema hivi: “Lengo la mradi huu ni kuwaandalia waabudu wenzetu wote walioathiriwa na dhoruba hiyo makao yanayofaa.” Haikuwa rahisi kufikia lengo hilo. Bw. Lainé anaeleza kwamba kuharibika kwa mifumo ya mawasiliano na barabara “kumefanya iwe vigumu kukamilisha kazi ya kutoa msaada.” Kufikia Aprili 20, nyumba 96 zilikuwa zimekamilika na nyingine 30 zimeanza kurekebishwa.

Smith Mathurin, makamu mwakilishi katika Bunge wa maeneo ya Paillant and Petite Rivière de Nippes.

Wenye mamlaka katika eneo hilo wametambua jitihada za Mashahidi katika kazi hiyo. Smith Mathurin, makamu mwakilishi katika Bunge wa maeneo yaliyoathiriwa sana ya Paillant na Petite Rivière de Nippes, anasema hivi: “Hata ingawa lengo kuu la Mashahidi wa Yehova ni kueneza habari njema, pia wamewasaidia wenye uhitaji.” Anaendelea kusema hivi: “Ninathamini mchango mkubwa wa Mashahidi wa Yehova baada ya Tufani Matthew. Tulihitaji msaada, na hamkubaki ndani ya kanisa lenu tu.”

Mwakilishi kutoka ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Haiti akionyeshwa paa jipya linalowekwa.

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova linasimamia kazi ya kutoa msaada kutoka makao yao makuu yaliyoko Warwick, New York, wakitumia pesa zilizochangwa kwa ajili ya kazi ya Mashahidi ya ulimwenguni pote ya kuwafundisha watu Biblia.

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

David A. Semonian, Ofisi ya Habari za Umma, +1-845-524-3000

Haiti: Daniel Lainé, +509-2813-1560