Hamia kwenye habari

OKTOBA 31, 2019
INDIA

Mashahidi wa Yehova Watoa Biblia ya Kitelugu Huko India

Mashahidi wa Yehova Watoa Biblia ya Kitelugu Huko India

Oktoba 25, 2019, Ndugu Ashok Patel, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya India, alitangaza kutolewa kwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kitelugu kwenye kusanyiko la eneo lililofanywa katika Ukumbi wa Hyderabad International Convention Centre huko Hyderabad, India.

Inakadiriwa kwamba watu milioni 91.9 huzungumza Kitelugu, na hivyo kuwa lugha ya tatu yenye wazungumzaji wengi zaidi nchini India baada ya Kihindi na Kibengali. Kwa sasa, kuna wahubiri 6,000 hivi wanaoutumia lugha ya Telugu, lakini jumla ya watu 8,868 walihudhuria kusanyiko. Mambo hayo yanaonyesha uwezekano wa ukuzi katika lugha hiyo, ambayo imekuwa na mizunguko miwili mipya mwaka huu.

Mradi wa kutafsiri Biblia hiyo ulichukua miaka mitano. Mmoja wa watafsiri aliyeshiriki alisema kwamba vijana hasa wanapata changamoto wanaposoma lugha ya zamani iliyotumiwa katika tafsiri nyingine za Biblia ya Kitelugu. “Kupitia tafsiri hii mpya, inaweza kusemwa kwamba sasa Yehova atazungumza na vijana akitumia lugha ya moja kwa moja na maneno ya kisasa yanayoeleweka kwa urahisi.” Mtafsiri mwingine aliongezea hivi, “Katika huduma, watu wataelewa kwa urahisi maandiko baada tu ya kuwasomea.”

Kwa kuongezea, kwa kuwa Biblia nyingi za Kitelugu zimeliondoa jina la Mungu, Yehova, kila mahali, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya itawasaidia wasomaji wa Kitelugu walifahamu jina la Mungu Mweza-Yote. Vilevile itawasaidia wasomaji waelewe maana ya awali ya maneno kama nafsi na roho, ambayo Biblia nyingine za Kitelugu zimeyatafsiri kulingana na itikadi za Kihindu.

Mhubiri mmoja alisema hivi, “Ninafikiri kwamba Biblia ya Kitelugu itawasaidia wasomaji wahisi upendo wa Yehova kuliko wakati mwingine wowote!” Ni wazi kwamba tafsiri hii mpya ya Kitelugu itawasaidia wasomaji ‘waonje na kuona kwamba Yehova ni mwema.’—Zaburi 34:8.