Hamia kwenye habari

OKTOBA 2, 2018
INDONESIA

Tetemeko la Ardhi na Tsunami Zaiharibu Sulawesi, Indonesia

Tetemeko la Ardhi na Tsunami Zaiharibu Sulawesi, Indonesia

Ijumaa, Septemba 28, tetemeko la ardhi lenye kipimo cha 7.5 lilitokea katika kisiwa cha Sulawezi huko Indonesia. Tetemeko hilo na tsunami iliyofuata, zilisababisha vifo vya watu zaidi ya 1,300. Wengi kati yao walikuwa katika jiji la Palu, lililoko Sulawesi ya Kati.

Ofisi ya tawi ya Indonesia, iliyoko Jakarta, inaripoti kwamba wahubiri wote 80 wanaoishi katika eneo liliathiriwa wako salama. Wachache kati yao walijeruhiwa na walihitaji kutibiwa hospitalini. Nyumba ya ndugu mmoja iliharibiwa kabisa na nyumba kadhaa za Mashahidi wengine ziliharibiwa kwa kadiri kubwa. Jengo linalotumiwa na Kutaniko la Palu kwa ajili ya mikutano liliharibiwa pia.

Dawati la Kutoa Msaada Wakati wa Misiba kwenye ofisi ya tawi linashirikiana na mwangalizi wa mzunguko na makutaniko ya karibu ili kuratibu jitihada za kutoa msaada. Kwa kuwa wahubiri katika eneo lililoathiriwa wana kiasi kidogo cha chakula, maji, na mahitaji mengine, ofisi ya tawi imepanga kwamba makutaniko matatu yaandae mahitaji hayo kwa ajili ya ndugu walioko Palu. Wazee wa huko wanashughulikia mahitaji ya kiroho, kihisia, na ya kimwili ya wahubiri. Mshiriki wa Halmashauri ya Tawi, mwangalizi wa Idara ya Ujenzi na Usanifu Majengo, pamoja na mwangalizi wa mzunguko wa eneo hilo watawatembelea wahubiri walioathiriwa ili kuandaa faraja na utegemezo.

Tunasali kwa ajili ya ndugu na dada zetu nchini Indonesia, tukitambua kwamba Yehova ataendelea kuwa ‘kimbilio lao na nguvu zao’ wakati huu wa taabu.—Zaburi 46:1.