Hamia kwenye habari

FEBRUARI 21, 2020
ISRAEL

Maandiko ya Kiebrania Yatolewa Katika Tukio la Pekee Huko Israeli

Maandiko ya Kiebrania Yatolewa Katika Tukio la Pekee Huko Israeli

Baba, mama pamoja na watoto wao wawili wakifurahia kupokea nakala za toleo jipya la Biblia

Ndugu Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza alianza kwa kusema: “Baraza Linaloongoza limeandaa zawadi ya pekee kwa ajili yenu,” alipokuwa akitoa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kiebrania katika Kiebrania cha kisasa. Jumla ya wahudhuriaji 2,125, walihudhuria tukio hilo la pekee lililofanyika Januari 11, 2020, katika uwanja wa Romema Arena uliopo huko Haifa, Israeli.

Ndugu David Simozrag, anayeratibu shughuli za Dawati la Habari za Umma nchini Israeli, alisema hivi: “Inakadiriwa kwamba kuna zaidi ya watu milioni nane katika eneo letu wanaozungumza Kiebrania. Tunaamini kwamba kutolewa kwa Tanakh a katika Kiebrania cha kisasa ni mchango wenye thamani katika jamii yetu.” Toleo hili jipya ni moja kati ya tafsiri chache sana za kisasa zinazopatikana leo katika Kiebrania.

Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, sasa inapatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 186. Kama vile waandishi wa maandishi ya Wamasora, ndugu zetu waliotafsiri Biblia hii walifanya kazi kwa bidii kufikisha ujumbe wa Biblia kwa usahihi. Timu hii ya watafsiri ilitumia zaidi ya miaka mitatu kumaliza tafsiri hii ya kisasa. Mmoja wa watafsiri hao alisema hivi: “Watu wengi wanaosoma Kiebrania walilazimika kutegemea ufafanuzi wa maandiko au tafsiri za lugha nyingine ili kuelewa mistari fulani au vitabu vyote vya Biblia. Biblia hii itawasaidia wasomaji wa kisasa kuelewa maana ya Maandiko.”

Familia ikionyesha Maandiko ya Kiebrania katika Kiebrania cha kisasa

Ndugu mmoja alisema: “Baada ya miaka mingi kupita ambayo msomaji wa kawaida asingeweza kuelewa sehemu kubwa za Tanakh, sasa anaweza kuelewa ujumbe wake ulio wazi na kwa usahihi.” Bila shaka , wahubiri 603 wanaozungumza Kiebrania kati ya wahubiri zaidi ya 2,000 katika eneo la ofisi ya tawi ya Israeli, watatumia zawadi hii ya pekee “kuichunguza Sheria ya Yehova na kuifuata”—Ezra 7:10.

a Tanakh ni ufupisho wa makundi matatu ya vitabu katika Maandiko ya Kiebrania. Vitabu hivyo vinapangwa katika mfuatano ambao ni tofauti na Biblia nyingi, yaani, Torah (Sheria), Nevi’im (Manabii), na Ketuvim (Maandishi). Herufi za kwanza za majina haya yanatokeza neno Tanakh. Biblia hii mpya pia inafuata mpangilio huu wa vitabu.