Hamia kwenye habari

Maonyesho ya “Wedontdothat” kwenye Kituo cha Elimu cha Ubinadamu

APRILI 28, 2022
ISRAEL

Maonyesho ya Mateso ya Mashahidi wa Yehova Mikononi mwa Wanazi Yafunguliwa Nchini Israel

Maonyesho ya Mateso ya Mashahidi wa Yehova Mikononi mwa Wanazi Yafunguliwa Nchini Israel

Machi 7, 2022, maonyesho kuhusu ujasiri wa Mashahidi wa Yehova ambao waliteswa na Wanazi yalifunguliwa nchini Israel. Maonyesho hayo yako katika Kituo cha Elimu cha Ubinadamu kwenye Jumba la Makumbusho la Ghetto Fighters lililo Magharibi mwa Galilaya. Maonyesho hayo yapo katika Kiarabu, Kiingereza, na Kiebrania. Yataendelea hadi Machi 2023. Ili kuandaa maonyesho hayo, wafanyakazi wa makumbusho walishirikiana na ndugu na dada zaidi ya 50 kutoka sehemu mbalimbali ulimwenguni. Ndugu na dada hao walisaidia katika kufanya utafiti kuhusu historia, kuandaa michoro ya kompyuta, na kutafsiri.

Kichwa cha maonyesho hayo ni “Wedontdothat,” maneno hayo yanamaanisha [“hatufanyi hivyo”]. Yanatokana na jina la utani ambalo mwanajeshi Mjerumani alimpa Ndugu Joachim Alfermann, Shahidi wa Yehova aliyefungwa na Wanazi. a Licha ya Wanazi kumtisha, kumpiga na kumfunga kwenye kambi ya mateso, Joachim alikataa kujiunga na jeshi la Ujerumani, na alisema: “Hatufanyi hivyo.” Msimamizi wa maonyesho hayo, Bi. Yaara Galor, alisema hivi: “Tunajua kwamba Wayahudi waliuawa kwa sababu mbalimbali. Hata hivyo, mamilioni ya watu wengine pia waliuawa. . . Vikundi vyote hivyo vilikuwa na hadithi za pekee.”

Mwingilio wa Kituo cha Elimu cha Ubinadamu

Dakt. Gideon Greif, ni msomi wa masuala ya Maangamizi makubwa ya Wayahudi na mwanahistoria anayechunguza hasa historia ya kambi ya mateso ya Auschwitz. Kwenye programu ya kufungua maonyesho hayo, alizungumzia kuhusu jinsi Mashahidi wa Yehova walivyokataa kutia sahihi azimio la kukana imani yao. Alisema: “Ilikuwa rahisi sana kwa [Mashahidi wa Yehova] kuachiliwa huru—walihitaji tu kuweka sahihi, jambo ambalo halingemaliza hata dakika moja. Hilo linaonyesha kwamba hata katika kipindi kigumu zaidi katika historia ya wanadamu, bado kuna watu ambao wanadumisha viwango vya juu vya maadili, kutia ndani maneno na matendo yao. Bila shaka Mashahidi wa Yehova wanastahili kuzungumziwa kwa njia hiyo, kukumbukwa, pia tunapaswa kujifunza kuwahusu na kufundishwa kuwahusu.”

Dada mmoja anayetumikia katika ofisi ya tawi nchini Israel ambaye alihudhuria programu ya kufungua maonyesho hayo alisema: “Machozi yalinilenga niliposhuhudia kwamba tuna maonyesho ya aina hii hapa Israel katika makumbusho yanayotembelewa na umma kwa ujumla . . . Siwezi kusahau jinsi wafanyakazi wa makumbusho hayo walivyokuwa wakiwataja jukwaani ‘Mashahidi wa Yehova’ katika Kiebrania. Kwa hakika, jina la Yehova lilitukuzwa katika maonyesho hayo.”

Ndugu David Simozrag kutoka ofisi ya tawi ya Israel akizungumza kwenye programu ya kufungua maonyesho hayo

Tuna hakika kwamba wale ambao watatembelea maonyesho hayo watajifunza kuhusu imani na ujasiri wa ndugu na dada zetu katika kipindi cha Wanazi nchini Ujerumani. Mfano mzuri wa imani unaweza kuwachochea watumishi wa Yehova leo waendelee ‘kukimbia kwa uvumilivu shindano la mbio.’​—Waebrania 12:1.