Hamia kwenye habari

SEPTEMBA 26, 2019
ITALIA

Uzinduzi wa Jiwe la Msingi la Kumbukumbu ya Mashahidi wa Yehova Walioteswa na Wanazi na Wafashisti Nchini Italia

Uzinduzi wa Jiwe la Msingi la Kumbukumbu ya Mashahidi wa Yehova Walioteswa na Wanazi na Wafashisti Nchini Italia

Jiwe la msingi limewekwa huko Risiera di San Sabba, Trieste. Mashahidi wa Yehova katika kambi za mateso walivaa pembetatu za zambarau katika sare zao

Mei 10  2019, maofisa wa serikali, wanahistoria, waandishi wa habari, na mamia ya wageni wengine walihudhuria tukio la uzinduzi wa jiwe la msingi la kumbukumbu ya maelfu ya ndugu na dada zetu ambao waliteswa na Wanazi na Wafashisti. Tukio hilo lilifanyika huko Risiera di San Sabba, Trieste, kaskazini-mashariki mwa Italia. Zamani, kambi hiyo ya mateso ilikuwa eneo la kupuria mpunga na pia kambi pekee yenye sehemu ya kuchomea maiti. Uzinduzi huo ulivutia vyombo vya habari katika eneo hilo na sehemu nyingine mojawapo ikiwa ni kituo kinachotazamwa zaidi nchini cha Canale 5.

Msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Italia Christian Di Blasio, alifungua tukio hilo kwa hotuba iliyokazia ushikamanifu. Alisema: “Ni Mashahidi wa Yehova peke yao walioteswa kwa sababu tu ya msimamo wao wa kidini chini ya Utawala wa Nazi. Wao ndio kikundi pekee cha kidini kilichokuwa na nafasi ya kuokoka kuuawa kwa sababu ya imani. Walihitaji tu kukana imani yao ya Kikristo na kuunga mkono utawala huo. Hata hivyo walikuwa na ujasiri wa kushikamana na viwango vyao vya Kikristo, yaani, kuwa washikamanifu kwa Mungu na upendo kwa wengine.” Kisha, Ndugu Di Blasio akaonyesha video ya mahojiano pamoja na Dada Emma Bauer, ambaye alisimulia kuhusu mateso ambayo yeye na familia yake walipitia wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Alisema kwamba Wakristo wa kweli hawatakana viwango vyao hata ikiwa watakufa. Katika umalizio wa tukio hilo, meya wa Trieste, Roberto Dipiazza, alihutubia wasikilizaji pia. Alisema: Ninafurahia sana uzinduzi huu. Tunahitaji kuhakikisha kwamba mateso ya aina hiyo hayajirudii tena. Kisha jiwe lilizinduliwa.

Wasomi wengi na watu maarufu walitoa maoni yao kuhusu umuhimu wa tukio hilo. Kwa mfano, Giorgio Bouchard, rais mstaafu wa Shirikisho la Makanisa ya Kievanjeli la Italia alisema: “Hakuna kanisa lolote lililowahi kulipa malipo ya damu ya hali ya juu sawa na Mashahidi wa Yehova. . . . Hata hivyo mateso haya hatari yameimarisha msimamo wao, ambao umejitokeza kuhukumu historia na tunaamini kwamba katika hukumu ya Mungu hili ndilo kanisa pekee la Kikristo ambalo lilipingwa kama kikundi na Utawala wa Nazi.” (Kwa maoni zaidi, tazama sandukku lililo chini.)

Inatazamiwa kwamba watu 120,000 watatembelea eneo hili la kihistoria la Risiera di San Sabba kila mwaka. Wageni wote watapata nafasi ya kuangalia jiwe hili likiwa kama kumbukumbu ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova ambao licha ya kupatwa na mateso ya Wanazi na Wafashisti, walidumisha imani yao na msimamo wao wa kutokuunga mkono upande wowote wa siasa.—Ufunuo 2:10.