Hamia kwenye habari

OKTOBA 21, 2016
ITALIA

Kampeni ya Mashahidi Yatoa Faraja Baada ya Tetemeko la Nchi Lililotokea Italia

Kampeni ya Mashahidi Yatoa Faraja Baada ya Tetemeko la Nchi Lililotokea Italia

ROMA—Katika mwezi wa Septemba 2016, Mashahidi wa Yehova walisambaza gazeti la Mnara wa Mlinzi lililokazia kuhusu faraja. Habari kuu ya gazeti hilo lenye kichwa “Unaweza Kupata Wapi Faraja?” ilikuwa habari ya msingi katika kampeni iliyofanywa ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova. Mashahidi wamefanya jitihada za pekee ili kuwafariji watu kwa kutumia Biblia katika eneo la katikati ya Italia, kwa kuwa Agosti 24, 2016, tetemeko kubwa la nchi lenye kipimo cha 6.2 lilitikisa miji ya Lazio, Marche, na Umbria. Tetemeko hilo lilisababisha vifo vya karibu watu 300 na kuacha watu zaidi ya 2,000 bila makao.

Christian Di Blasio, msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Italia, anasema: “Kampeni hii ya ulimwenguni pote ilikusudiwa kuwapa faraja watu katika nchi zote wanaokabili hali zozote zile. Lakini hapa Italia, tunazingatia hasa hali ngumu inayowakumba waathiriwa wa tetemeko hili la nchi na pia wale wanaofanya kazi ya kutoa msaada.”

Mashahidi wa Yehova wakizungumza na mtu aliyeathiriwa na tetemeko la nchi kwenye mji wa Amatrice, ambako watu wengi zaidi waliathiriwa.

Ingawa kuna makutaniko 15 ya Mashahidi wa Yehova kwenye eneo lililokumbwa na tetemeko, hakuna Shahidi aliyekufa au kuumia vibaya. Hata hivyo, nyumba tatu za Mashahidi ziliharibiwa vibaya, na nyingine zinahitaji marekebisho madogo. Bw. Di Blasio alisema kwamba hata baadhi ya Mashahidi ambao nyumba zao ziliharibiwa walijitolea kuwafariji majirani wao wakitumia gazeti hilo. Isitoshe, Mashahidi ambao walikuwa wameokoka tetemeko la nchi lililotokea zamani kidogo walijitolea kuzungumza na waathiriwa. Bw. Di Blasio anasema: “Wajitoleaji hao walisema kwamba ujumbe wa Biblia umewachochea na kuwapa faraja maishani mwao, na wanataka kufanya yote wawezayo kushiriki ujumbe huu wa faraja na watu wengine katika jamii ambao wanateseka.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

David A. Semonian, Ofisi ya Habari za Umma, 1-718-560-5000

Italia: Christian Di Blasio, 39-06-872941