Hamia kwenye habari

Picha: Mahubiri ya umma jijini Prague, Jamhuri ya Cheki. Kulia: Viwanja vya michezo vilivyo Ostrava (juu) na Prague (Chini) ambako michezo ya magongo yalifanyika

JUNI 28, 2024
JAMHURI YA CHEKI

Mahubiri ya Umma Kwenye Shindano la Kimataifa la Mchezo wa Magongo wa Kuteleza Kwenye Barafu Katika Jamhuri ya Cheki

Mahubiri ya Umma Kwenye Shindano la Kimataifa la Mchezo wa Magongo wa Kuteleza Kwenye Barafu Katika Jamhuri ya Cheki

Kuanzia Mei 10 hadi 26, 2024, Shindano la Kimataifa la Mchezo wa Magongo wa Kuteleza Kwenye Barafu lilifanyika katika Jamhuri ya Cheki. Watu 800,000 hivi walihudhuria, katika jiji la Ostrava na jiji la Prague. Mashahidi wa Yehova waliweka vigari vya machapisho nje ya viwanja wakati wa michezo hiyo. Zifuatazo ni baadhi ya ripoti zenye kutia moyo.

Vijana wawili walikaribia kigari cha machapisho na kwa fadhili wakawauliza akina ndugu wao ni akina nani na walikuwa wakifanya nini hapo. Akina ndugu waliwaeleza vijana hao kuhusu kazi ya Mashahidi wa Yehova na wakawaeleza jinsi funzo la Biblia linavyoongozwa. Mmoja kati ya vijana hao aliuliza kuhusu wakati na mahali ambapo funzo hilo huongozwa. Akina ndugu walimweleza kwamba funzo hilo linaweza kuongozwa wakati na mahali panapomfaa. Kijana huyo alikubali kujifunza Biblia.

Katika pindi tofauti, wanaume watatu walizungumza na ndugu zetu na walishangaa sana kusikia kwamba Mashahidi wa Yehova hawalipwi chochote wanaposhiriki katika huduma. Mwanamume mmoja aliuliza hivi: “Ikiwa hamlipwi, ninyi binafsi mnapata faida gani kwa kufanya kazi hii?” Mashahidi wa Yehova waliwafafanulia jinsi mafundisho ya Biblia yalivyoboresha maisha yao na kuwapatia tumaini la wakati ujao. Mwanamume mmoja alivutiwa sana na majibu ya ndugu zetu, na akasema kwamba angependa kujifunza mengi zaidi na akaomba broshua Furahia Maisha Milele!

Mwanamume mwingine alipita mara kadhaa mahali ambapo kigari chetu cha machapisho kilipokuwa. Hatimaye alisimama na kuwauliza akina ndugu: “Kuna tofauti gani kati ya imani yenu na kile kinachofundishwa kanisani kwangu?” Akina ndugu walitumia Biblia kumfafanulia kwa ufupi kuhusu imani ya Mashahidi wa Yehova. Mwanamume huyo alisikiliza kwa makini sana na akashukuru sana kwa ufafanuzi wa wazi waliompa. Kisha akina ndugu wakamwonyesha baadhi ya habari zinazopatikana kwenye jw.org na jinsi ya kutumia tovuti hiyo kujifunza mengi zaidi kuhusu Biblia na mafundisho yake.

Tunathamini sana bidii ya ndugu na dada zetu wa Jamhuri ya Cheki ya kushiriki “habari njema ya mambo mema” na wale wote waliokuwa tayari kusikiliza.​—Waroma 10:15.