Hamia kwenye habari

JUNI 6, 2018
KAZAKHSTAN

Siku 441 za Kifungo—Mahojiano na Teymur na Mafiza Akhmedov

Siku 441 za Kifungo—Mahojiano na Teymur na Mafiza Akhmedov

Baada ya kupata msamaha wa rais wa Kazakhstan, Nursultan Nazarbayev, Ndugu Teymur Akhmedov aliachiliwa Aprili 4, 2018. Alifungwa kwa siku 441. Wenye mamlaka walimkamata kwa kuwaeleza wengine imani yake ya kidini.

Muda mfupi baada ya Teymur kuachiliwa kutoka gerezani, mwakilishi wa Habari za Ofisi ya Umma (OPI) katika makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova yaliyoko Warwick, New York, alizungumza naye pamoja na mke wake, Mafiza, ambao sasa wamerudi nyumbani kwao huko Astana, mji mkuu wa Kazakhstan. Habari hii imefupishwa na kuelezwa kwa njia iliyo wazi.

OPI: Kwanza, tungependa kujua mengi kukuhusu Ndugu Akhmedov. Umekuwa Shahidi wa Yehova lini?

Teymur Akhmedov: Nilibatizwa Oktoba 9, 2005. Kabla ya kujifunza kweli, sikuamini kwamba kuna Mungu. Kwa miaka mingi, sikumwamini yeyote au chochote. Baadaye, mke wangu alianza kujifunza, nilitaka kujua wanazungumzia nini na Mashahidi. Kwa hiyo, nilisimama nyuma ya mlango na kuwasikiliza bila wao kujua.

Niliposikia mambo waliyojifunza, nilipendezwa kwa sababu walizungumzia kuhusu fadhili na mambo mema tu. Mwishowe, Mashahidi walinitambulisha kwa Ndugu Veslav, ambaye ni raia wa Poland lakini alikuwa akitumikia nchini Kazakhstan. Siku ya kwanza alipokuja, nilimwambia: ‘Nitakuuliza swali moja tu. Nikiridhishwa na jibu lako, tutakuwa marafiki na kuendelea kujifunza. Hata hivyo, nisipopenda jibu lako, usihisi vibaya, lakini sitaendelea kujifunza.’ Kisha nikamwuliza Ndugu Veslav kile kinachowapata wafu. Alifungua Biblia kwenye andiko la Mhubiri 9:5 na kuniambia, ‘Soma mstari huu na utajua kinachotokea.’ Niliposoma mstari huo, niligundua kwamba hii ndiyo kweli. Nilikubali arudi tena na kunifundisha Biblia.

Kwa hiyo, ukajifunza na mwishowe ukabatizwa mwaka wa 2005.

Sasa tusonge mbele hadi kabla ya kukamatwa. Mei 2016 ulikutana na kikundi cha wanaume waliodai kwamba wanapendezwa na mafundisho ya Mashahidi wa Yehova. Kwa miezi michache, mlikutana mara kadhaa ili kuzungumzia Biblia. Ukifikiria mazungumzo hayo, kuna chochote ambacho kilifanya uwatilie shaka?

TA: Ndiyo, niliwaeleza kwamba kawaida tunajifunza Biblia na mtu mmoja-mmoja, si na kikundi. Nilipendekeza kwamba kila mmoja ajifunze peke yake, lakini kila mara nilipopopendekeza, walikataa na kusema kwamba wanafurahia kujifunza wakiwa kikundi. Pia, mara kadhaa, walialika watu wengine wajiunge nasi na kuniomba nirudie mambo tuliyojifunza awali.

Mafiza Akhmedov: Siku moja, nilijiunga na funzo hilo la Biblia. Niligundua kwamba walikuwa wakizungumzia dini mbalimbali, ingawa walikuwa wamejifunza kwa muda. Pia, niliona kwamba chumba walichokodi kilikuwa cha bei ghali kuliko uwezo wa wanafunzi. Niliwaambia kwamba waliishi maisha mazuri isivyo kawaida kwa wanafunzi. Hawakufurahishwa na maneno yangu. Tulipokuwa tukiondoka, walimwita Teymur na kumwambia hawangependa nirudi siku nyingine. Wakati huo nilikuwa nikingoja nje.

Ulijua lini kwamba wanaume uliojifunza nao hawakupendezwa na Mashahidi wa Yehova bali walikuwa wakishirikiana na polisi wa siri, Kamati ya Usalama wa Taifa (KNB)?

TA: Niligundua kwamba wanashirikiana na KNB nilipokuwa nikisikiliza kesi mahakamani.

Ulihisije ulipokamatwa na baadaye kuhukumiwa kwamba “unachochea mgawanyiko wa kidini” na kupendekeza “[dini yako] kuwa bora”?

TA: Kwa kweli, nilipokamatwa nilifikiri watanipeleka kwenye kituo cha polisi ili kufafanua habari niliyozungumzia, kisha waniachilie. Nilikuwa tayari kujitetea na kueleza mambo niliyozungumza nao.

Nilishangazwa na jinsi hali ilivyokuwa mwishowe, lakini sikuogopa. Nilishangaa waliponishtaki kwa kuchochea chuki ya kidini na msimamo mkali. Mashahidi wa Yehova wanawaambia wengine kuhusu Yehova na hawajawahi kuhusianishwa na chuki au mgawanyiko. Nilikuwa na uhakika kabisa kwamba sikuwa na hatia na kwamba Yehova angenitegemeza. Ni kweli kwamba nilikuwa na wasiwasi, lakini nilikumbuka ushauri huu kutoka katika Biblia; ‘Mtupe mahangaiko yenu yote juu ya Yehova, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’—1 Petro 5:7.

Baadaye, Mei 2, 2017, baada ya kuwa mahabusu kwa miezi mitatu, mahakama ya wilaya ya Astana akatoa hukumu ya miaka mitano na marufuku ya miaka mitatu baada ya hapo kuhusu kushiriki elimu ya Biblia. Hukumu hiyo ilikuathirije?

TA: Mahakama ilipotangaza uamuzi wake, nilifikiri ningelazimika kutumikia kifungo changu chote. Nilikuwa na mtazamo huu: ‘Ikiwa hili ni jaribu, basi Yehova anadhibiti muda na anajua litaisha lini.’ Niliazimia kusubiri hadi mwisho.

Kituo cha kurekebisha tabia katika jiji la Pavlodar, Kazakhstan, ambako Ndugu Akhmedov alifungwa.

Tulisikia kwamba ulikuwa na hali mbaya ya afya ulipofungwa. Ni kweli?

TA: Ndiyo, nilikuwa mgonjwa na nilikuwa nikipata matibabu kabla ya kufungwa. Nilipokamatwa, sikupata tena matibabu na ugonjwa ukaanza kusambaa.

Mafiza, ulijihisije wakati huo?

MA: Niliogopa na kushuka moyo sana. Ilikuwa vigumu kwangu kufanya maamuzi baada ya Teymur kufungwa kwa sababu kwa miaka 38 tuliyofunga ndoa, hatukuwa tumetenganishwa hata mara moja. Lakini Teymur alinifariji na kuniambia: ‘Usiwe na wasiwasi! Yehova atatupa miaka 25 zaidi katika mfumo huu ili kulipia miaka 5 ambayo tutatenganishwa!’

Ni nini kingine kilichokusaidia mume wako akiwa gerezani?

MA: Ndugu na dada walinisaidia sana. Teymur alipofungwa, kwa kweli nilifikiri kila mtu ataogopa kunitembelea kwa sababu ya hali zilizofanya Teymur afungwe. KNB walikuwa wakifuatilia utendaji wetu na mambo yaliyofanyika nyumbani kwetu.

Kisha siku moja, mzee na mke wake wakaja kunitembelea, niliimarishwa sana. Nilipowauliza, ‘Hamkuogopa kunitembelea?’ Walijibu, ‘Kwa nini tuogope? Siku hizi wenye mamlaka wanaweza kutufuatilia kupitia simu zetu. Hivyo, wakitaka, wanaweza kutupata kwa urahisi.’

Wazee walinifanyia ziara ya uchungaji na kunitia moyo nisishindwe na jaribu bali niwe imara kiroho.

Teymur, ni nini kilichokusaidia kuvumilia jaribu hili na kuwa na mtazamo unaofaa?

Ndugu Akhmedov akiwa amefungwa pingu kwenye kitanda cha hospitali huko Almaty muda mfupi kabla ya kuachiliwa huru. Ingawa mwanzoni alikatazwa kupata matibabu, wenye mamlaka walimruhusu apate matibabu hali yake ilipozorota.

TA: Sala kwa Yehova! Nilisali kila siku kupata mwongozo, uelewaji, na nguvu ili niendelee kuwa na shangwe, ushikamanifu, na auminifu chini ya hali hizi ngumu. Niliona waziwazi jibu lake kwa sala zangu. Alinitegemeza, na sikuwahi kuhisi kwamba niko peke yangu gerezani.

Pia, usomaji wa Biblia ulinisaidia. Katika gereza moja, ningeweza kupata Biblia wakati wowote. Katika gereza lingine, kulikuwa na Biblia kwenye maktaba ya gereza, hivyo ningeweza kwenda na kuisoma mara moja kwa juma.

Pia nilikumbuka maneno ya ndugu niliyejifunza naye Biblia. Alizoea kusema kwamba hatupaswi kuogopa tunapokabili changamoto. Nakumbuka nilimwuliza: ‘Kwa nini sipaswi kuogopa? Namna gani ikiwa changamoto ni kubwa na inaogopesha?’ Alisema kwamba Yehova hawezi kuruhusu tujaribiwe kupita tunavyoweza kuhimili na kwamba atatupa nguvu tunazohitaji kushinda jaribu lolote. (1 Wakorintho 10:13) Hivyo, nikiwa gerezani sikusahau kamwe wazo hilo la Kimaandiko.

Ulihisije ulipogundua kwamba ndugu ulimwenguni pote walijua hali yako na kwamba walikuwa wakisali kwa ajili yako?

TA: Kwa hakika nilihisi mkono wa Yehova ukinitegemeza kwa sababu hili ni tengenezo lake. Hilo lilinihakikishia kwamba sitaachwa na siku moja Yehova atanikomboa.

Inashangaza kwamba niliogopa sana wazo la kuwa gerezani. Niliogopa magereza. Niliposoma kuhusu ndugu zetu walio gerezani, nilikuwa nikisali, ‘Yehova tafadhali, nisaidie nisifungwe gerezani!’ Lakini wakati huohuo, nilikuwa na tamaa kubwa ya kuwatembelea watu gerezani na kuwaambia kuhusu kweli. Nilipoomba kuwahubiria wafungwa, ndugu waliniambia kwamba kwa sasa hatuna ruhusa ya kutembelea magereza nchini Kazakhstan. Hivyo, nilipokuwa mahakamani nilikuwa na hisia kadhaa. Kwa upande mmoja, niliogopa. Lakini wakati huohuo, nilihisi kwamba ndoto yangu ya kuwahubiria wafungwa huenda ikatimia.

Kwa hiyo, je, ulipata fursa ya kuwahubiria wafungwa?

TA: Ndiyo. Pindi moja, niliitwa na ofisa mmoja ambaye alitaka kuzungumza nami. Nilipoingia ofisini mwake, alisema, ‘Ninajua wewe ni Shahidi wa Yehova, hivyo, hata usifikirie kunihubiria!’ Nikamjibu, ‘Sina nia ya kufanya hivyo.’ Kisha akauliza, ‘Jina la Mungu ni nani?’ Nikamwambia, ‘Jina la Mungu ni Yehova.’ Akasema, ‘Basi, Yesu ni nani? Yeye si Mungu?’ Nikamwambia, ‘Hapana, ni mwana wa Mungu.’ Kisha akauliza, ‘Basi kwa nini Wakristo wa Kanisa Othodoksi wanaamini kwamba ni Mungu?’ Nikamwambia, ‘Ni vema ukiwauliza wenyewe.’

Siku nyingine, nilifaulu kuongea na watu 40 au zaidi wakati uleule. Mwanasaikolojia alikuja gerezani kutembelea wafungwa. Tulikuwa tukizungumzia ndoa alipouliza maoni yetu kuhusu ndoa za wake wengi. Kila mtu alikuwa na nafasi ya kutoa maoni yake.

Niliporuhusiwa kuzungumza, nilisema kwamba sina maoni kuhusu mada hiyo lakini napenda maoni ya mtu mwingine ambayo ningependa kuwaeleza. Kisha nikasema: ‘Ndiyo sababu mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, nao watakuwa mwili mmoja.’ (Mwanzo 2:24) Mwanasaikolojia huyo akauliza, ‘Hayo ni maoni ya nani?’ Nikajibu, ‘Ni maoni ya Yehova Mungu, yule aliyewaumba wanadamu. Linataja watu wawili tu; si zaidi.’

Kisha akauliza, ‘Je, una sababu nyingine ya kufikiri kwamba mume anapaswa kuwa na mke mmoja?’ Nikanukuu Mathayo 7:12, ambayo inasema: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima ninyi pia mwatendee vivyo hivyo.” Nikasema: ‘Hayo ni maneno ya Yesu. Tafadhali waulize wanaume walio hapa ikiwa wangependa mke wao awe na mume mwingine. Ikiwa wanaume hawataki wake zao wawe na mume mwingine, basi wanawake hawataki waume zao wawe na wake wengi.’ Mwanasaikolojia huyo alisema kwamba kati ya majibu yote alipenda jibu langu zaidi.

Inatia moyo kujua kwamba licha ya hali yako ngumu, ulipata nafasi za kuwahubiria watu wanaokuzunguka!

Baada ya mahakama kukataa rufaa kadhaa za kuomba uachiliwe, kutia ndani rufaa iliyopelekwa kwenye Mahakama Kuu ya Kazakhstan, ilionekana kana kwamba kwa msingi wa sheria hakukuwa na lingine la kufanya.

Hata hivyo, ungeweza kuachiliwa ikiwa ungetia sahihi hati fulani. Tueleze kuhusu hilo na kwa nini ulikataa kutia sahihi?

TA: Kwa kweli walipendekeza hilo mara kadhaa. Ingawa lilionekana kuwa tendo la fadhili, hati hiyo ilisema kwamba nilikuwa na hatia ya mashtaka yote niliyoshtakiwa na kwamba nilijutia matendo yangu. Baadaye, niliambiwa kwamba ningeweza kuandika hati ya kukiri kosa na kuomba msamaha. Wenye mamlaka walinishauri niandike kwamba nilikuwa nimekosea kuwaambia wengine kuhusu imani yangu lakini sasa nilijutia matendo yangu na ninaomba kuachiliwa kwa sababu ya hali yangu ya afya.

Nilikataa kukiri kuwa na hatia na nikawaambia wenye mamlaka kwamba ni bora nikae gerezani nikiwa na dhamiri safi badala ya kuachiliwa na niwe na dhamiri mbaya.

Kwa kweli tunathamini mfano wako wa imani na kwamba ulikataa kuvunja dhamiri yako.

Mwishowe, mambo yalibadilika kwa njia isiyotarajiwa. Unaweza kutuambia jinsi ulivyopata habari kwamba utasamehewa na kuachiliwa kutoka gerezani?

TA: Siku moja mlinzi alikuja kuniambia kwamba nimepigiwa simu. Nakumbuka nikijiuliza, ‘Ni nani anayeweza kunipigia simu?’ Nilipopokea simu hiyo, mwanamke fulani alijitambulisha na kuniambia kwamba angekuja gerezani kuniachilia huru. Sikujua niseme nini. Hivyo, tulipomaliza kuongea, niliamua kumwambia mwanangu, kwa kuwa sikutaka kumshtua mke wangu na habari hizo au kumpa tumaini la uwongo.

Nilipomaliza kuongea na simu, mlinzi aliniuliza, ‘Umeambiwa nini?’ Nikamwambia inaonekana mtu ananitania kwa kuwa mwanamke aliyepiga simu ameniambia anakuja kuniachilia huru.

Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, akiwa na Teymur na Mafiza Akhmedov muda mfupi baada ya Ndugu Akhmedov kuachiliwa.

Mlinzi akaniambia kwamba si utani, kile alichosema ni kweli.

Mafiza, uliitikiaje ulipopata habari hizo?

MA: Mwana wangu aliponiambia, mimi pia nilifikiri ni utani. Tulikuwa tumesubiri muda mrefu sana kupata habari hizo!

Tunaweza tu kuwazia jinsi mlivyohisi mlipokutana kwa mara ya kwanza zaidi ya mwaka mmoja baada ya Teymur kukamatwa!

Sasa ukitafakari uliyopitia, umejifunza nini kutokana na jaribu hili la imani?

MA: Nakumbuka jinsi nilivyolia kuhusu hali ya Ndugu Bahram [Hemdemov] na [Dada] Gulzira Hemdemov. [Ndugu Hemdemov alikamatwa na wenye mamlaka nchini Turkmenistan Machi 2015. Mei 19, 2015, alihukumiwa kifungo cha miaka minne kwa mashtaka ya uwongo ya “kuchochea chuki ya kidini” na bado hajaachiliwa.] Hata kabla ya Teymur kukamatwa, nilifikiria jinsi Gulzira anavyokabili hali ngumu. Sasa, ningependa kumkumbatia na kumtumia upendo mchangamfu na utegemezo. Kwa kuwa nimekabili hali hii ngumu na Teymur, ningependa kumwambia kwamba ninamsikitikia kwa sababu ya maumivu aliyo nayo. Ninajua kwamba, kama mimi, anamtegemea Yehova na ndugu wamtegemeze.

Ninawashukuru sana ndugu wote waliotutegemeza, ndugu katika kutaniko letu na makutaniko yote ulimwenguni pote, Baraza Linaloongoza, mawakili, na wana wetu.

Ndugu Akhmedov akiwa ameshika cheti cha msamaha baada ya kuachiliwa.

TA: Ninaweza kusema jambo moja tu. Kila mtu lazima akabili jaribu fulani. Bila shaka, si kila mtu atafungwa gerezani. Kwa watu fulani, jaribu huenda likawa kunyanyaswa na mshiriki wa familia ambaye si mwamini. Kwa wengine, huenda ni kushughulika na ndugu au dada ambaye si rahisi kushughulika naye. Hata tuwe tunakabili changamoto gani, kila mmoja anahitaji kuchagua ikiwa atafuata kanuni za Mungu au atazipuuza. Tukifuata kanuni, tutashinda majaribu kwa mafanikio. Jambo bora ni kuikubali hali yetu na kukumbuka kwamba Yehova atatupatia nguvu za kukabiliana na jaribu hilo.

Ninaishukuru sana familia yangu na wana wangu ambao wamenitegemeza. Walitumia kila fursa kunitembelea na hilo lilinisaidia kubaki imara.

Isitoshe, ninataka kuwashukuru ndugu ulimwenguni pote kwa yote waliyofanya. Nilithamini sala zao, na barua zao zenye kutia moyo. Sikuwahi kuhisi kwamba niko peke yangu. Kilichonipata kimeongeza upendo wangu kwa ndugu ulimwenguni pote na kuimarisha uhusiano wangu na Yehova.