Hamia kwenye habari

JANUARI 27, 2015
KAZAKHSTAN

Biblia Mpya ya Kikazakh Yatolewa Kusanyikoni na Kuonyeshwa Kwenye Siku ya Wageni

Biblia Mpya ya Kikazakh Yatolewa Kusanyikoni na Kuonyeshwa Kwenye Siku ya Wageni

Gerrit Lösch mshiriki wa Baraza Linaloongoza akitoa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kikazakh.

ALMATY, Kazakhstan—Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kikazakh ilitolewa kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova lililofanywa Septemba 26-28, 2014. Wahudhuriaji wote 3,721 walipata nakala ya Biblia hiyo mpya.

Dakt. Alexander Garkavets, mtafiti wa maneno ya Kituruki, alieleza hivi kuhusu Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kikazakh: “Licha ya upungufu wa habari za kuwasaidia kutafsiri Biblia katika Kikazakh, Mashahidi wamefanya kazi nzuri sana. Wanastahili pongezi nyingi kwa jinsi walivyofunua njia mpya za kueleza mawazo katika Kikazakh kutoka lugha nyingine. Biblia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatumia lugha ya kisasa na hivyo inaeleweka kwa watu wote.”

Siku ya wageni: Mashahidi waliweka kibanda cha asili (traditional yurt) ambapo viburudisho viliandaliwa.

Juma lililofuata kusanyiko hilo, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Kazakhstan iliwaalika watu kwenye siku ya wageni Oktoba 3, ambapo Biblia mpya ya Kikazakh ilionyeshwa. Redio ya Kazakhstan inayoitwa Azattyq ilieleza hivi: “Ofisi hiyo ilitembelewa na wenye mamlaka wa Akimat (serikali ya utawala ya kimkoa) wa jiji la Almaty, wakiongozwa na mkuu wa Idara ya Mambo ya Kidini, Bw. Nurzhan Zhaparkul, mwakilishi wa wajumbe kutoka nchi za kigeni, wataalamu wa masomo ya kidini, na wengine.” Bw. Zhaparkul alieleza hivi: “Mashahidi wa Yehova walitukaribisha vizuri sana katika ofisi yao ya Almaty. Wanastahili pongezi kwa kutualika na kufanya hivyo kunatusaidia sana katika kazi yetu.”

Nurzhan Zhaparkul (katikati), mkuu wa Idara ya Mambo ya Kidini, na viongozi wengine kutoka kamati ya kidini watembelea ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova kwenye siku ya wageni.

Mialiko ya siku ya wageni katika ofisi ya tawi ilisambazwa jijini Almaty.

Msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Kazakhstan, Polat Bekzhan, alieleza hivi: “Tumefurahi kuona watu wengi wakihudhuria kusanyiko letu mwaka huu na pia kuona Biblia ya Kikazakh ikipokewa vizuri katika jamii yetu yenye watu wengi wanaozungumza Kikazakh. Lengo letu la kuandaa siku ya wageni lilitimia, kwa sababu viongozi serikalini, vyombo vya habari, na majirani wetu walipata fursa ya kuwafahamu vizuri zaidi Mashahidi wa Yehova.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1 718 560 5000

Kazakhstan: Polat Bekzhan, simu +7 727 232 36 62