Hamia kwenye habari

SEPTEMBA 4, 2019
KENYA

Mashahidi wa Yehova Watoa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Katika Kijaluo Nchini Kenya

Mashahidi wa Yehova Watoa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Katika Kijaluo Nchini Kenya

Mashahidi wa Yehova walitoa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kijaluo kwenye kusanyiko la eneo huko Kisumu, Kenya, mnamo Agosti 30, 2019. Ndugu Remy Pringle, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Kenya, alitangaza kutolewa kwa Biblia hiyo kwenye siku ya kwanza ya kusanyiko la eneo. Kulikuwa na idadi ya wahudhuriaji 2,481, kutia ndani makusanyiko mengine mawili yaliyounganishwa.

Kazi ya kutafsiri Biblia hiyo ilichukua karibu miaka mitatu. Mojawapo ya watafsiri walioshiriki kuitafsiri alisema: “Itawasaidia sana akina ndugu na dada ambao wametamani kupata Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kijaluo. Familia nyingi katika makutaniko yetu hazina uwezo wa kuwanunulia Biblia washiriki wote wa familia zao, na hivyo itakuwa baraka kubwa kwa kila mmoja wao kupata Biblia. Vilevile, lugha ya kisasa iliyotumiwa katika tafsiri hii itafanya funzo la kibinafsi na ibada ya familia kuwa yenye kuimarisha imani zaidi.”

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imetafsiriwa ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 184, kutia ndani matoleo mazima 25 yaliyorekebishwa ambayo yanategemea toleo la 2013. Tuna hakika kwamba Biblia hiyo itawasaidia wahubiri 1,800 hivi wanaozungumza Kijaluo katika eneo la ofisi ya tawi ya Kenya wazidi kumkaribia Yehova. Vilevile itasaidia katika kazi ya kuwahubiria kikamili, zaidi ya watu milioni 5 wanaozungumza Kijaluo.—Mathayo 24:14.