Hamia kwenye habari

Kushoto: Ndugu akitumia kifaa cha kielektroni kuwaelekeza wageni waliotembelea banda letu kwenye jw.org. Picha ndogo: Mwingilio wa Maonyesho ya Vitabu ya Kimataifa Jijini Bogotá, nchini Kolombia

JUNI 6, 2024
KOLOMBIA

Umuhimu wa Elimu ya Biblia Wazungumziwa Katika Maonyesho ya Vitabu ya Kimataifa Nchini Kolombia

Umuhimu wa Elimu ya Biblia Wazungumziwa Katika Maonyesho ya Vitabu ya Kimataifa Nchini Kolombia

Maonyesho ya Vitabu ya Kimataifa yamefanyika jijini Bogotá, nchini Kolombia, kuanzia Aprili 17 hadi Mei 2, 2024. Waandaaji wa maonyesho hayo wanaripoti kwamba zaidi ya watu 600,000 kutoka nchi 25 walihudhuria maonyesho hayo. Wakati wa maonyesho hayo, Mashahidi wa Yehova waliweka banda lenye machapisho ili kuwasaidia watu kujifunza kuhusu umuhimu wa Biblia na ujumbe wa tumaini.

Ndugu na dada wakishiriki ujumbe wa Biblia na watu mbalimbali waliotembelea banda letu

Mwanamume mmoja alikaribia banda letu na akasema kwamba Mashahidi wa Yehova walitembelea familia yao alipokuwa mdogo. Alisema kwamba bado alivutiwa kujifunza mengi kumhusu Mungu na ujumbe wa Biblia. Ndugu yetu alimwonyesha jinsi funzo la Biblia linavyoongozwa kwa kutumia kitabu Furahia Maisha Milele! Kisha, akamwonyesha mwanamume huyo jinsi ya kutafuta mkutano wa kutaniko ulio karibu na mahali anapoishi na jinsi anavyoweza kuomba mtu amtembelee kupitia jw.org. Siku chache baadaye ndugu zetu walifurahi sana kujua kwamba mwanamume huyo amepakua JW Library kwenye kifaa chake, amehudhuria mikutano ya mwisho juma, na tayari kuna ndugu ambaye ameanza kujifunza Biblia na mwanamume huyo.

Mama na mwana wake wakionyeshwa jinsi funzo la Biblia linavyoongozwa

Mama mmoja na mwana wake mdogo walipokaribia banda letu, mvulana huyo mdogo alivutiwa sana kutazama video kutoka kwenye mfululizo Uwe Rafiki ya Yehova. Mama wa mvulana huyo alimwomba mmoja wa dada zetu amwonyeshe mahali ambapo anaweza kununua video hizo zenye kufundisha kwa ajili ya mwana wake. Dada yetu alimweleza kwamba video hizo zinapatikana bila malipo kwenye jw.org, pamoja na machapisho mengine yanayotegemea Biblia ambayo yametayarishwa kwa kusudi la kuwasaidia vijana kuwa na maadili mazuri na kumkaribia Mungu. Baada ya kutazama video kadhaa na mwana wake, mama huyo alithamini sana ubora wa video hizo na masomo ambayo zinafundisha. Alikubali akina dada wamwonyeshe jinsi funzo la Biblia linavyoongozwa, na mipango ikafanywa ili kuendeleza mazungumzo na mwanamke huyo.

Tunashangilia pamoja na ndugu na dada zetu nchini Kolombia kwa fursa hii ya pekee ambayo wamepata ya kuwasaidia wengine kujifunza ‘kutembea katika nuru ya Yehova.’​—Isaya 2:5.