Hamia kwenye habari

Ndugu watatu kati ya watano nchini Korea waliotangazwa kuwa hawana hatia na Mahakama ya Wilaya ya Jeonju.

JANUARI 23, 2019
KOREA KUSINI

“Hawana Hatia”

Mara ya Kwanza Katika Historia ya Korea Kusini, Mahakama Imeamua Wanaokataa Kujiunga na Jeshi kwa Sababu ya Dhamiri Hawana Hatia

“Hawana Hatia”

Kwa mara kwanza katika historia ya Korea Kusini, waendesha-mashtaka wa serikali waliomba mahakama ya rufaa itangaze kwamba ndugu watano waliokataa kujiunga na jeshi hawana hatia. Kwa sababu hiyo, mahakama iliamua kwamba ndugu hao hawakuwa na hatia na hawapaswi kushtakiwa tena kuhusu jambo hilo. Uamuzi huo unafutilia mbali maamuzi ya mahakama za chini ambazo ziliwahukumu ndugu zetu kwa kukwepa utumishi wa kijeshi.

Maamuzi hayo ya kutokuwa na hatia, yaliyotangazwa Desemba 14, 2018, yaliweka msingi wa kuwaondolea hatia ndugu zaidi ya 900 walio na kesi zinazosubiri uamuzi katika mahakama mbalimbali nchini Korea. Akina ndugu walioondolewa mashtaka watasubiri kuanzishwa kwa mpango wa utumishi wa badala wa kiraia utakaowawezesha kutumikia jamii badala ya kujiunga na jeshi.

Mahakama ya rufaa ilitoa uamuzi wake kwa kutegemea maamuzi mawili ya kihistoria yaliyofanywa katika mwaka wa 2018 na Mahakama ya Kikatiba ya Korea na Mahakama Kuu ya Korea. Maamuzi hayo yalikomesha sera iliyokuwepo kwa miaka 65 iliyoonyesha kwamba mtu yeyote anayekataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri anapaswa kufungwa mara moja, hata ikiwa ana sababu inayofaa ya kidini.

Maamuzi hayo mawili ya mahakama hizo kuu, yanayotambua kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri kuwa ni haki ya msingi, yalisifiwa sana na mashirika ya haki za kibinadamu. Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu ya Korea ilisema hivi: “Uamuzi wa kauli moja wa Mahakama Kuu umesitisha historia mbaya ya kuwaadhibu kama wahalifu watu wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri, ambayo ilianza katika miaka ya 1950, na kuwaathiri watu 20,000 hivi  . . . Tunasikitika sana kwamba watu waliokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri pamoja na familia zao walilazimika kuvumilia hali hizo ngumu.”

Sasa, watu wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri wanapaswa kuthibitisha kwamba uamuzi wao unategemea imani “yenye kina, imara, na ya unyoofu.” Mahakimu wameagizwa wachunguze ikiwa kwa unyoofu mtu anayekataa kujiunga na jeshi anaamini mambo anayosema. Mahakama Kuu ilisema, “Kila sehemu ya maisha yake . . . inapaswa kuongozwa na imani hiyo.” Kwa hiyo, ndugu zetu wanapojibu maswali ya mahakimu, wana nafasi ya kutoa ushahidi kuhusu uamuzi wao wa kibinafsi wa kujiepusha na vita na utumishi wa kijeshi.—1 Petro 3:15.

Kwa zaidi ya miaka 60, Mashahidi wa Yehova nchini Korea wamevumilia kufungwa gerezani kwa msimamo wao unaotegemea dhamiri. Uamuzi wao unathibitisha kwamba tukiwa Wakristo hatuungi mkono upande wowote katika mambo ya kijeshi kwa sababu tunataka sana kutii amri kuu ya pili, ya ‘kumpenda jirani yetu kama tunavyojipenda wenyewe.’—Mathayo 22:39.