Hamia kwenye habari

Lee Gyo-won, ni Shahidi wa Yehova anayetumikia kifungo cha miezi 18 katika Gereza la Daegu kwa kukataa kujiunga na jeshi. Akiwa pamoja na Mashahidi wengine zaidi ya 100 waliofungwa gerezani, wanasubiri kesi ya umma itakayofanywa Agosti 30 kwenye Mahakama Kuu ili kushughulikia suala la kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri.

AGOSTI 24, 2018
KOREA KUSINI

Kesi ya Mahakama Makuu Inapokaribia, Aliyekataa Kujiunga na Jeshi Apata Tumaini

Kesi ya Mahakama Makuu Inapokaribia, Aliyekataa Kujiunga na Jeshi Apata Tumaini

SEOUL, Korea Kusini—Januari 2017, Lee Gyo-won, ambaye alikuwa na umri wa miaka 21 wakati huo, alisimama mbele ya hakimu wa Korea Kusini akiwa na matumaini na alijihami kwa maneno yaliyochaguliwa vizuri. Bw. Lee alikuwa na lengo la kumsadikisha hakimu kwamba kukataa kwake utumishi wa kijeshi hakukuwa uhalifu bali uamuzi uliochochewa na dhamiri uliotegemea imani yenye nguvu ya kuepuka ukatili.

Bw. Lee, wa dini ya Mashahidi wa Yehova ambao ni Wakristo, hakuwa na sababu ya kuwa na matumaini. Kesi yake ilipoenda kusikizwa, Mashahidi 392 waliokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri walikuwa gerezani wakiwa wamehukumiwa vifungo ambavyo vikijumlishwa vilifikia miaka 588. Tangu mwaka wa 1950, waamini wenzake zaidi ya 19,340 wamefungwa gerezani vifungo ambavyo vikijumlishwa vinafikia miaka 36,800 kwa sababu sheria ya Korea haikuwa imeona msimamo wao kuwa msingi unaofaa wa kukataa utumishi wa kijeshi.

Hata hivyo, tangu mwaka wa 2004, mahakimu ambao hawakufurahishwa na desturi ya kuwafunga wale wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri, waliamua katika kesi 90 kwamba hawakuwa na hatia. Mmoja wao, Jaji Choi Jong-du wa Mahakama ya Rufaa ya Busan aliona kwamba uamuzi wa kibinafsi wa kutojiunga na utumishi wa kijeshi “unategemea ‘dhamiri’ yenye nguvu inayochochewa na imani ya kidini.”

Hatimaye, mnamo Juni 2018, Mahakama ya Kikatiba ya Korea Kusini ilitoa uamuzi kwamba Sheria ya Utumishi wa Kijeshi inapaswa kuandikwa upya ili kuwe na uwezekano wa kufanya utumishi wa badala wa kiraia. * Lakini uamuzi huo wa kihistoria haukufanywa kwa wakati uliomfaa Bw. Lee. Anaeleza hivi: “Ingawa nilifanya yote ninayoweza kukata rufaa, sasa nimefungwa katika Gereza la Daegu.” Anatumikia kifungo cha miezi 18.

Bw. Lee anajiunga na kikundi cha Mashahidi wengine wengi waliokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri tangu siku za utawala wa Wajapani. Vijana wawili Mashahidi nchini Japani walipofungwa mnamo 1939 kwa kukataa kujiunga na jeshi, serikali ya Japani iliwakamata Mashahidi wengine nchini Japani, Taiwan, na Korea (ambayo wakati huo ilijulikana kama Chosun). Mashahidi 38 waliofungwa nchini Korea walikataa kumtukuza maliki wa Japani kwa njia ya pekee na kufanya chochote kilichohusiana na vita. Mashahidi watano kati ya waliofungwa walikufa kwa ukatili, na wengi waliwekwa huru kwa sababu tu Japani ilishindwa mnamo 1945.

Baadhi ya Mashahidi wa Yehova 19,340 ambao wamewahi kufungwa kwa sababu ya dhamiri.

Mashahidi wamekuwa wakikataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri kwa zaidi ya karne moja. Kwa kutegemea Biblia na mfano uliowekwa na Wakristo wa mapema, Mashahidi wanaamini kwamba Wakristo wanapaswa should kuepuka vita kwa sababu hawana haki ya kuua mwanadamu. Isitoshe, Mashahidi hawaungi mkono upande wowote wa mambo ya kisiasa kwa sababu wanajiona kuwa raia wa Ufalme, au serikali ya Mungu.

Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu ndipo kwa mara ya kwanza Mashahidi (ambao wakati huo walijulikana kuwa International Bible Students) walipingwa kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi. Nchini Uingereza, Mashahidi 400 hivi walikataa kujiunga na jeshi hata ingawa serikali ilisema ni lazima wafanye hivyo. Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Mashahidi nchini Marekani walifanyiza kikundi kikubwa zaidi cha wafungwa waliokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri, kwani 4,400 hivi walifungwa.

Huenda mfano bora zaidi unaoonyesha usadikisho imara wa Mashahidi ni yale mateso waliyovumilia chini ya serikali ya Wanazi. Inakadiriwa kwamba Wanazi waliwaua Mashahidi 400 hivi, wengi wao kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Mashahidi zaidi ya 1,000 walikufa kwa sababu ya kuteswa na pia kwa sababu ya ukatili katika kambi na gerezani kwa sababu ya kushikamana na imani yao. Kulingana na mwanahistoria Robert Gerwarth, wao ndio “kikundi pekee kilichoteswa na Serikali ya Wanazi kwa msingi wa imani yao ya kidini tu.”

Hata hivyo, Mashahidi nchini Korea ndio wamevumilia kwa muda mrefu zaidi kwa sababu ya msimamo unaotegemea dhamiri. Lee Gyo-won, ambaye baba yake alikufa katika aksidenti alipokuwa na umri wa miaka minane, alifundishwa na mama yake kuhusu Biblia na umuhimu wa kufuata dhamiri yake. Bw. Lee anasema hivi: “Nilipoelewa kwa nini tuliumbwa, nilichochewa kumpenda Mungu wangu, Yehova. Kuanzia wakati huo niliazimia kumtumikia na kumtanguliza Yehova katika maisha yangu yote.”

Akifahamu kwamba huenda atafungwa, Bw. Lee alichagua kujifunza kazi ya ujenzi. Alipanga kujiajiri baada ya kutoka gerezani, kwa kuwa alitambua kwamba rekodi ya kifungo chake ingefanya iwe vigumu kwake kuajiriwa.

Bw. Lee anasema hivi kuhusu siku aliyoenda mahakamani, “Nilikuwa na hamu ya kuthibitisha kwamba sikuwa na hatia, kwa sababu nilifanya uamuzi huo kwa unyoofu kwa kutegemea imani na dhamiri yangu.” Alitafakari kuhusu Stefano na Paulo, Wakristo wa mapema ambao walitetea imani yao kwa ufasaha walipofikishwa mahakamani. Bw. Lee anasema hivi, “Nafikiri nilizungumza vizuri zaidi kuliko nilivyokuwa nimejitayarisha.”

Agosti 30, 2018, Mahakama Kuu ya Korea Kusini itasikiliza kesi mbele ya umma ili kuchunguza maagizo yaliyotolewa na Mahakama ya Kikatiba ya kutoa utumishi wa badala wa kiraia kwa ajili ya watu wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Uamuzi wa mahakama hiyo kuu utaathiri sana kesi 900 zinazosubiri katika mahakama mbalimbali. Mbali na hilo, Mashahidi 117, kutia ndani Bw. Lee bado wako gerezani wakisubiri ombi lao la kupata msamaha wa rais wa Korea Kusini likubaliwe. Ingawa huenda kufikia Agosti 30 Bw. Lee akawa bado katika Gereza la Daegu, atafuatilia kesi hiyo kwa makini sana.

Licha ya kufungwa na rufaa yake kukataliwa, Bw. Lee anatumaini kwamba mambo yatakuwa mazuri zaidi kwa waabudu wenzake: “Ninatumaini kwamba nitakuwa kati ya [Mashahidi] wa mwisho kufungwa gerezani, kifungo ambacho nimepata kwa sababu ya kuwapenda wengine, na muhimu zaidi, kwa sababu ya kumpenda Mungu na kanuni zake.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

Paul S. Gillies, Ofisi ya Habari za Umma, +1-845-524-3000

Korea Kusini: Hong Dae-il, +82-31-690-0055