Hamia kwenye habari

Makao Makuu ya Tume ya Haki za Kibinadamu za Kitaifa yaliyoko jijini Seoul, South Korea

JANUARI 25, 2017
KOREA KUSINI

Tume ya Haki za Kibinadamu ya kitaifa Yasihi Uhuru wa Dhamiri Uheshimiwe

Tume ya Haki za Kibinadamu ya kitaifa Yasihi Uhuru wa Dhamiri Uheshimiwe

Desemba 9, 2016, Tume ya Haki za Kibinadamu ya Korea Kusini ilitoa maoni yake kuhusiana na kesi za walalamikaji zinazoshughulikiwa na Mahakama ya Katiba. Maoni hayo yalichanganua haki ya kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Ikitoa sababu zake kwa kutegemea viwango vya karibuni zaidi vya haki za kibinadamu, Tume hiyo ilifikia mkataa kwamba uhuru wa dhamiri ni haki ya msingi ya kibinadamu ambayo haipaswi kuwekewa vizuizi na inapaswa kulindwa na serikali.

Ni muhimu kutambua kwamba maoni ya Tume hiyo yanaonyesha kwamba haki hii ya msingi ya kibinadamu ni “sababu halali” ya kutoshiriki katika utumishi wa kijeshi. Tume hiyo ilisihi serikali ipatanishe viwango vya katiba kuhusu uhuru wa dhamiri na wajibu wa kutumikia jeshini kwa kuandaa “utumishi wa badala wa kiraia ambao utakuwa na manufaa kwa jamii.”

Maoni hayo yalionyesha kwamba zoea la kuwafunga wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri halitimizi kusudi lolote. Tume hiyo ilisema hivi: “Adhabu inapaswa kuwa na matokeo ya kukomesha au kuzuia makosa ya uhalifu. Hata hivyo, watu wengi wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri hawajutii uamuzi waliofanya wala kubadili uamuzi wao kwa sababu ya kuogopa adhabu. . . . Basi adhabu hiyo haina matokeo yoyote kwao.”

Tume hiyo ilikazia tena uamuzi wake uliofanywa Desemba 26, 2005, kwamba Jamhuri ya Korea inapaswa ianzishe utumishi wa badala wa kiraia ambao utazingatia haki za wale wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri na wajibu wa kulinda taifa upatanishwe. a Kwa kuwa Tume hiyo ina mamlaka ya kutetea haki za kibinadamu, iliwasilisha maoni yake kwenye Mahakama ya Katiba ili iyajadili.

“Haki ya kukataa kujiunga na utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri inalindwa na uhuru wa dhamiri unaoelezwa kwenye Katiba na sheria za kimataifa za haki za kibinadamu. Kuwaadhibu wale wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri kwa madai ya kukiuka Sheria za Utumishi wa Kijeshi wakati kuna njia za kuwaruhusu wafanye wajibu wao wa kulinda taifa kupitia utumishi wa badala wa kiraia ni kuingilia uhuru wa dhamiri.”—Uamuzi wa Tume ya Haki za Kibinadamu ya Kitaifa ya Novemba 28, 2016.

Nafasi ya Kufanikiwa

Akitoa maoni yake kuhusu uamuzi wa Tume, Profesa wa Sheria Jae-seung Lee alisema hivi: “Ikiwa serikali ya Korea Kusini itaamua kwamba itaheshimu ‘haki ya kibinadamu ya kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri, huenda ikaamua kuanzisha utumishi wa badala wa kiraia. Ikiwa itafanya hivyo, ninapendekeza kwamba izingatie viwango vya kimataifa vya utumishi wa badala wa kiraia, ili kuwe na nafasi ya kutosha ya kufanikiwa kwa mpango huo.”

Dae-il Hong, msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini humo, alisema hivi: “Tangu Agosti 2012, Mahakama ya Katiba ilipochukua hatua tena ya kuchunguza jambo hili, zaidi ya vijana 2000 wa Mashahidi wa Yehova walikuwa wamefungwa gerezani. Tunatarajia kusikia uamuzi wa Mahakama ya Katiba unaopatana na viwango vya kimataifa ambavyo vinaheshimu maisha na amani ya watu. Tunatumaini kwamba barabara za kwenda gerezani zitafungwa na vijana Mashahidi wataweza kutumikia jamii kwa njia ambayo haipingani na dhamiri zao.”

a Julai 11, 2008, Tume ya Haki za Kibinadamu ya Kitaifa kwa mara ya pili ilimsihi Waziri wa Ulinzi wa Taifa kuanzisha na kuendeleza utumishi wa badala wa kiraia kwa ajili ya wale wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Kwa kuongezea, Tume ilituma maoni yake Novemba 26, 2007, kupinga zoea linalojirudia la kuwaadhibu askari wa akiba wanaokataa kupata mazoezi ya kijeshi kwa sababu ya dhamiri.