Hamia kwenye habari

DESEMBA 9, 2013
KOREA KUSINI

Korea Kusini Yawatenganisha Waliofungwa kwa Sababu ya Dhamiri Kutoka kwa Wafungwa wa Uhalifu

Korea Kusini Yawatenganisha Waliofungwa kwa Sababu ya Dhamiri Kutoka kwa Wafungwa wa Uhalifu

Mashahidi wa Yehova ambao wamefungwa gerezani huko Korea Kusini kwa kukataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri wamepata kitulizo kutoka kwa serikali ya nchi hiyo. Kitulizo cha aina gani? Sasa Mashahidi hao hawawekwi pamoja katika chumba kimoja cha gereza na wafungwa wa uhalifu.

Nchi ya Korea Kusini ilichukua hatua hiyo baada ya mkutano uliofanyika Desemba 2012 baina ya wawakilishi wa Mashahidi wa Yehova katika nchi hiyo na ofisa mmoja wa ngazi za juu anayeshughulika na Huduma za Kurekebisha Watu Tabia nchini Korea. Kati ya wawakilishi hao kulikuwa pia na baba mmoja ambaye kwa wakati huo mwanaye alikuwa akitumikia kifungo gerezani. Wawakilishi hao wa Mashahidi wa Yehova waliwasilisha hangaiko lao wakielezea kwamba Mashahidi vijana huwekwa katika gereza moja na wahalifu sugu. Miezi mitano baada ya mkutano huo, asilimia 70 ya Mashahidi waliofungwa gerezani walitenganishwa na wafungwa wa uhalifu na kuwekwa katika gereza moja na Mashahidi wenzao.

Historia ndefu sana ya kuwafunga gerezani wanaokataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri. Kwa muda mrefu serikali ya Korea Kusini imekuwa ikiwafunga Mashahidi wa Yehova gerezani kwa sababu ya kufuata mwongozo au kanuni ya Biblia ya kukataa kutumia silaha. Kufikia sasa, takriban Mashahidi 600 hivi wanatumikia vifungo vyao gerezani kwa kukataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri. Kwa kipindi cha miaka 60 iliyopita zaidi ya Mashahidi 17,000 wamefungwa gerezani kwa sababu wamekataa utumishi huo wa lazima, ambao ni takwa kwa kila mwanamume mwenye umri wa kati ya miaka 19 na 35.

Si jambo linaloshangaza kuona watu wa vizazi kadhaa vya Mashahidi katika familia moja ambao wameshtakiwa, wamehukumiwa, na kufungwa gerezani kama wahalifu. Seungkuk Noh, Shahidi wa kizazi cha pili katika familia yake alikamilisha kifungo chake cha miaka mitatu mnamo mwaka wa 2000. Anasema hivi: “Nilifungwa katika gereza lilelile alilofungwa babangu alipokuwa kijana—na hali katika gereza hilo hazijabadilika tangu enzi zake.” Leo kwa wastani muda ambao mtu anayekataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri anaweza kufungwa, ni mwaka mmoja na nusu. Serikali ya Korea Kusini bado haijafanya mipango ya kuwa na utumishi mwingine wa badala usiohusisha mambo ya kijeshi.

Ho Gyu Kang alikuwa na umri wa miaka 21 alipofungwa gerezani kwa sababu ya kukataa kusajiliwa jeshini. Kwa mara ya kwanza maishani mwake alitenganishwa na watu wa familia yake. “Niliogopa sana na nilikuwa na wasiwasi mwingi,” anakumbuka Bw. Kang. Yeye pamoja na vijana wengine Mashahidi walifungwa katika gereza moja pamoja na wafungwa wengine ambao walionwa kuwa wahalifu sugu wasioweza kubadilika. Baadhi ya wahalifu hao walifungwa gerezani kwa sababu walikuwa katika magenge ya wahalifu na pia walikuwa wameua.

Kuanzia siku wanapofungwa jela hadi siku wanapoachiliwa huru, wafungwa Mashahidi ambao wengi wao wana umri mdogo kwa kulinganisha na wafungwa wengine, huteswa kimwili na kihisia. Mazingira hayo hufanya iwe vigumu kwa wafungwa Mashahidi kutekeleza kwa uhuru mambo yanayohusu kumwabudu Muumba wao kama vile kusali na kujifunza Biblia kibinafsi. Mwaka baada ya mwaka kwa makumi ya miaka, vijana wengi Mashahidi walivumilia mateso kutoka kwa wafungwa wa uhalifu.

Kuwatenganisha wafungwa kunapatana na sheria za kimataifa. Kwa kuwatenganisha wafungwa wengi Mashahidi na kuwaweka katika gereza lingine lisilo na wafungwa wa uhalifu, serikali ya Korea Kusini imetenda kupatana na Kifungu cha 8 katika Sheria ya Umoja wa Mataifa Kuhusu Jinsi ya Kuwatendea Wafungwa. Serikali ya Korea Kusini imechukua mkondo uliofuatwa na nchi ya Ugiriki zaidi ya miaka 20 iliyopita ambayo ni mojawapo ya nchi iliyo katika Muungano wa Ulaya. Wizara ya Ulinzi na Wizara ya Haki ya nchi hiyo ziliidhinisha kwamba Mashahidi ambao wamefungwa gerezani kwa kukataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri wasiwekwe pamoja na wafungwa wengine. Katika mwaka wa 1992, Wizara ya Ulinzi iligeuza kambi ya kijeshi ya Sindos, Thessalonica, iwe gereza kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova pekee. Ripoti moja rasmi ilisema kwamba “roho ya ufikirio inayoonyeshwa na Wizara ya Ulinzi, kuwaelekea wafungwa wenye hali za kipekee [Mashahidi wa Yehova],” ilichangia sana katika uamuzi wa kuwatenganisha wafungwa Mashahidi kutoka kwa wafungwa wengine na kuwaweka katika gereza moja. Tangu mwaka wa 1998 serikali ya Ugiriki iliacha kabisa kuwafunga gerezani Mashahidi waliokataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri.

Vivyo hivyo, serikali ya Korea Kusini imeonyesha roho ya ufikirio kwa kuwatenganisha Mashahidi vijana waliofungwa kutoka kwa wafungwa wengine, vijana ambao wamefungwa gerezani kwa sababu ya imani yenye nguvu katika mafundisho ya Biblia. a Tayari kufikia sasa, magereza na vituo kadhaa vya wafungwa vyenye Mashahidi wengi nchini Korea Kusini vimefaulu kutekeleza mpango huo, na angalau kwa sasa wafungwa wa masuala ya dhamiri wako katika mazingira salama zaidi. Akieleza kuhusu faida za mpango huo, Shahidi mmoja aliyefungwa katika Gereza la Gunsan anasema: “Angalau hatuko chini ya uvutano mbaya kama vile ukosefu wa maadili na matusi. Sasa tunaweza kufurahia mazungumzo ya kiroho yenye kujenga pamoja na ndugu zetu Mashahidi.”

‘Sasa hatuko chini ya uvutano mbaya na tunaweza kufurahia mazungumzo yenye kujenga’

Tatizo la muda mrefu la kutoheshimu msimamo wa wanaokataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri. Ingawa serikali ya Korea Kusini inastahili pongezi kwa hatua iliyochukua hivi karibuni ya kuwatenga wafungwa ambao ni Mashahidi kutoka kwa wafungwa wengineo, serikali hiyo bado haijafaulu kufuata kielelezo kilichowekwa na nchi nyingine ambazo zimefaulu kabisa kusuluhisha suala hilo. Kwa mfano, tangu mwaka wa 1997 nchi ya Ugiriki imefaulu kuanzisha utumishi wa badala wa kiraia usiohusisha mambo ya kijeshi, utumishi ambao hufanywa na wale ambao dhamiri zao zinawazuia wasifanye utumishi wa kijeshi. Mwanzoni, nchi ya Ujerumani ilikuwa imeanzisha utumishi wa aina hiyo kwa ajili ya wale ambao dhamiri zao haziwaruhusu wafanye utumishi wa kijeshi lakini tangu mwaka wa 2011 nchi hiyo iliamua kwamba utumishi wa kijeshi si wa lazima tena. Katika mwaka wa 2000, nchi ya Taiwan ilipitisha sheria ya kuwepo kwa utumishi wa badala kwa ajili ya wale wanaokataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri.

Mashahidi vijana na familia zao nchini Korea Kusini wanatumaini kwamba punde si punde nchi yao pia itaanza kufuata viwango vya sasa vya kimataifa kuhusu suala muhimu linalohusu haki ya msingi ya binadamu ya kuwa na uhuru wa dhamiri.

a Sheria ya kimataifa ambayo serikali ya Korea inapaswa kufuata, inatambua kwamba kukataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri ni haki ya msingi ya binadamu. Tazama makala yenye kichwa “Jamii ya Kimataifa Yalalamikia Ukosefu wa Haki wa Korea Kusini.”