Hamia kwenye habari

Majengo ya ofisi ya tawi yaliyoko Lilongwe, Malawi. Picha ndogo (kuanzia juu kushoto): Ndugu Bill McLuckie, mtumishi wa kwanza wa ofisi ya tawi ya Malawi; Wenye mamlaka wakitaifisha ofisi ya tawi mwaka wa 1967; Dada akishiriki katika kazi ya kuhubiri hivi karibuni akiwa na shangwe

DESEMBA 28, 2023
MALAWI

Miaka 75 Imepita Tangu Ofisi ya Kwanza ya Tawi Ilipoanzishwa Nchini Malawi

Historia Yenye Kustaajabisha ya Uvumilivu

Miaka 75 Imepita Tangu Ofisi ya Kwanza ya Tawi Ilipoanzishwa Nchini Malawi

Kufikia 2023, miaka 75 imepita tangu ofisi ya kwanza ya tawi ilipoanzishwa nchini Malawi katika mji wa Blantyre mwaka wa 1948.

Kabla ya hapo, Malawi ilikuwa chini ya ofisi ya tawi ya Afrika Kusini. Mwanzoni mwa miaka ya 1930, idadi ya ndugu na dada iliongezeka pole kwa pole kutoka watu 28 tu katika mwaka wa 1934 hadi zaidi ya watu 5,600 katika mwaka 1948. Kwa kuwa idadi ya Mashahidi iliongezeka, ofisi ya kwanza ya tawi ilifunguliwa Septemba 1, 1948 kwenye nyumba ndogo iliyokodishwa katika mji wa Blantyre. Ofisi hiyo ilitumiwa hadi mwaka wa 1958, majengo mapya ya Betheli yalipojengwa karibu na hapo.

Kushoto: Watafsiri wa Kichichewa na Kichitumbuka wakiwa mbele ya ofisi ya tawi iliyojengwa Malawi mwaka wa 1958. Miongoni mwao ni Baston Nyirenda (aliyetiwa alama), sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Malawi. Kulia: Baston, mwenye umri wa miaka 80, akiwa na mke wake, Violet leo

Majengo hayo yalitumiwa kwa karibu miaka kumi kabla ya wenye mamlaka nchini humo kupiga marufuku utendaji wa Mashahidi wa Yehova Oktoba 1967 na kutaifisha majengo hayo. Licha ya hilo, akina ndugu waliokuwa wakiongoza waliendelea kuratibu kazi ya kuhubiri na kuwasaidia ndugu na dada nchini pote. Kwa karibu miaka 26, Mashahidi wa Yehova waliteswa kikatili na kutendewa kwa jeuri kwa njia mbaya sana kwa sababu hawakuunga mkono upande wowote wa kisiasa. Katika kipindi hicho, ndugu na dada zetu walifungwa, waliteswa kikatili, na hata kuuawa. Baadhi ya ndugu na dada waliamua kukimbilia nchi jirani kama vile Msumbiji, Zambia, na Zimbabwe.

Ndugu na dada wakifanya kazi ya kutafsiri machapisho yanayotegemea Biblia katika Kichichewa

Marufuku hiyo iliondolewa Agosti 12, 1993. Kisha kwa miaka miwili iliyofuata, akina ndugu nchini Zambia ambao walisimamia kazi iliyofanywa nchini Malawi kwa miaka kadhaa wakati wa marufuku, walisaidia kupanga kazi. Kisha, ndugu zetu walinunua nyumba mbili jijini Lilongwe kwa ajili ya ofisi mpya ya tawi ya Malawi. Mwaka wa 1994, Baraza Linaloongoza liliidhinisha mpango wa kutafuta eneo litakalofaa la kujenga majengo mapya ya Betheli nchini humo. Mei 19, 2001, majengo hayo yaliwekwa wakfu na programu hiyo ilihudhuriwa na zaidi ya ndugu na dada 2,000. Wengi kati yao walikuwa wale waliovumilia mateso kwa miaka mingi wakiwa washikamanifu. Ndugu Trophim Nsomba ambaye alikuwa mwangalizi wa mzunguko wakati wa marufuku, alikuwa miongoni mwa waliohudhuria programu hiyo ya wakfu. Ndugu Nsomba alisema hivi akitafakari kuhusu majengo hayo mapya na ukuzi wa kiroho aliouona nchini Malawi: “Hizi baraka kutoka kwa Yehova ni zenye kustaajabisha hivi kwamba mimi na [mke wangu] tunahisi ni kama tunaota ndoto!”

Leo, kuna makutaniko 1,924 nchini Malawi na kuna ndugu na dada zaidi ya 109,000. Idadi hiyo inatia ndani ndugu na dada 225 wanaotumikia katika ofisi ya tawi iliyoko Lilongwe, inayosimamia kazi ya kutafsiri machapisho ya Biblia katika lugha saba.

Wachache kati ya ndugu na dada 109,000 wanaomtumikia Yehova kwa ushikamanifu leo nchini Malawi

Tunasali kwamba Yehova aendelee kuwabariki ndugu na dada zetu nchini Malawi wanaojipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu kwa kuvumilia kwa miaka mingi.​—2 Wakorintho 6:4.