Hamia kwenye habari

NOVEMBA 15, 2018
MAREKANI

Moto wa Msituni Waathiri California

Moto wa Msituni Waathiri California

Habari za karibuni zaidi: Ofisi ya tawi ya Marekani imethibitisha habari ya kusikitisha kwamba ndugu mwenye umri wa miaka 70 kutoka Paradise, Kaskazini ya California, amekufa kutokana na moto wa msituni unaoitwa Camp Fire.

Mioto mitatu ya msituni katika jimbo la California, Marekani, imesababisha madhara makubwa na vifo vya watu 48 hivi. Moto mkubwa zaidi, ambao unaitwa Camp Fire, unaendelea kuteketeza eneo la California Kaskazini, na kufikia sasa eneo lenye ukubwa wa ekari 117,000 limeteketezwa na majengo 7,100 yameharibiwa. Majengo mengi yaliyoharibiwa ni nyumba za watu. Katika eneo la California Kusini, mioto miwili, yaani, Hill Fire na Woolsey Fire, imeteketeza eneo lenye ukubwa wa ekari 94,500 na kuharibu majengo 435 hivi. Kulingana na ripoti moja, eneo lote lililoteketezwa na moto wa msituni katika jimbo la California mwaka huu “ni eneo kubwa kuliko nchi ya Ubelgiji na Luxembourg.”

Ripoti za kwanza kutoka ofisi ya tawi ya Marekani zinaonyesha kwamba moto wa Camp Fire umewalazimisha wahubiri 427 hivi wahame kutoka Chico na Paradise. Inasikitisha kwamba dada mwenye umri mkubwa kutoka Kutaniko la Ponderosa amekufa kutokana na moto huo. Isitoshe, imethibitishwa kwamba, kufikia sasa, nyumba 94 zimeharibiwa kabisa au kwa kiwango kikubwa. Pia, Jumba moja la Ufalme huko Paradise limeharibiwa.

Kutokana na moto wa Hill na Woolsey, wahubiri 420 hivi katika majiji ya Oxnard, Simi Valley, na Thousand Oaks wamehamishwa. Inasikitisha kwamba ndugu mmoja pamoja na mama yake ambaye si Shahidi walikufa huko Malibu walipokuwa wakiukimbia moto. Uchunguzi wa mapema unaonyesha kwamba nyumba 21 za ndugu zetu pamoja na jumba moja la Ufalme zimeharibiwa.

Ofisi ya tawi imeanzisha Halmashauri za Kutoa Msaada ili kutunza mahitaji ya ndugu zetu. Chini ya mwongozo wa waangalizi wa mzunguko, wazee wanaandaa ziara za uchungaji na msaada kwa ndugu ambao wameathiriwa na moto wa msituni. Jumamosi, Novemba 10, kulikuwa na programu ya pekee jijini Chico kwa ajili ya ndugu na dada zaidi ya 270 walio huko. Mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani na waangalizi wa mzunguko waliwatia moyo akina ndugu kwa kutumia Maandiko.

Tunasali kwamba ndugu na dada zetu wanaokabili hali hiyo ngumu wafarijiwe na kuimarishwa na Yehova na wakumbuke kwamba hivi karibuni sana atafuta machozi yetu yote na kumeza kifo milele.—Isaya 25:8.