Hamia kwenye habari

JUNI 1, 2016
MAREKANI

Mashahidi wa Yehova Wanauza Jengo la Kihistoria la The Towers Katika Eneo la Brooklyn

Mashahidi wa Yehova Wanauza Jengo la Kihistoria la The Towers Katika Eneo la Brooklyn

Towers Hotel kama ilivyoonekana zamani.

NEW YORK—Mei 24, 2016, Mashahidi wa Yehova walitangaza rasmi mpango wa kuuza jengo la ghorofa 16 liitwalo The Towers lilililopo mtaa wa 21 Clark Street kwenye Eneo la Kihistoria la Brooklyn Heights. Jengo hilo lenye ukubwa wa kilomita za mraba 29,150 ambalo zamani lilikuwa hoteli, limekuwepo katika eneo hilo la Brooklyn kwa miaka 90 hivi. Linajulikana sana kwa sababu ya minara yake minne iliyo juu ya jengo hilo.

Awali jengo hilo liliitwa Leverich Towers Hotel iliyofunguliwa katika mwaka wa 1928. Ramani ya ujenzi wa jengo hilo ilichorwa na kampuni ya wasanifu-majengo mashuhuri ya Starrett & Van Vleck, ambao ndio waliochora ramani za ujenzi wa maduka makubwa zaidi ya kampuni kama vile Lord & Taylor na pia Saks Fifth Avenue yaliyoko New York City. Baada ya miaka michache, hoteli hiyo ilibadilishwa jina na wamiliki wapya na kuitwa Towers Hotel (Hoteli Yenye Minara). Jengo hilo lilikuwa na mapambo yenye mtindo ulio na asili ya Kiroma, ukumbi wenye shada za taa zenye mapambo, na eneo juu ya jengo hilo ambapo mtu anaweza kufurahia mandhari ya Lower Manhattan, Bandari ya New York, na Daraja la Brooklyn. Jengo hilo lilisemekana kuwa “Mfalme wa Hoteli za Brooklyn.”

Ngazi ya kifahari ya The Towers iliyo na uzio uliotengenezwa kwa mbao za mkangazi. Juu yake kuna tao tatu na mchoro wenye kuvutia.

Licha ya kwamba mwanzoni hoteli hiyo ilikuwa maarufu, kufikia miaka ya 1970 ilihitaji kurekebishwa. Mashahidi walinunua jengo hilo Januari 14, 1975. Kufikia mwaka wa 1978, walikuwa wamerekebisha jengo hilo na lilikuwa likitumiwa kama jengo la makazi na chumba cha kulia chakula kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova 1,000 waliokuwa wakifanya kazi kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote. Richard Devine, msemaji wa Mashahidi, anasema hivi: “Kazi ya uchapishaji ilikuwa ikiongezeka haraka. Jengo hilo lilitupatia nafasi tuliyohitaji kwa ajili ya wafanyakazi wetu waliokuwa wakiongezeka.”

Ukiwa kwenye eneo la juu la jengo hilo, unaweza kuona ofisi za makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi, daraja la Brooklyn na la Manhattan, pamoja na jengo la Empire State Building.

Kuanzia mwaka wa 1995, Mashahidi wa Yehova walianza ukarabati mkubwa wa jengo hilo ili lirudie ubora wake wa awali. Bw. Devine aliifafanua kazi hiyo ya ujenzi hivi: “Miaka ya 1990, tulijenga upya sehemu ya ndani ya jengo hilo na kuweka mfumo mpya wa maji na umeme. Mbali na hilo tulijenga ngazi ya kifahari inayotoka juu kwenye eneo kuu la mapokezi hadi kwenye chumba cha kulia chakula.”

David A. Semonian, msemaji wa Mashahidi kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote, alisema hivi: “Unapotembea kwenye mitaa ya Brooklyn Heights na kufika karibu na jengo hilo la The Towers, lazima utatekwa na umaridadi wake. Lakini mbali na umaridadi huo ambao tumejitahidi sana kuutunza, jengo hilo la The Towers limetumika kama makazi mazuri ya washiriki wa makao yetu makuu kwa makumi ya miaka.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

David A. Semonian, Ofisi ya Habari za Umma,simu 1-718-560-5000