Hamia kwenye habari

JULAI 10, 2013
MAREKANI

Mashahidi wa Yehova Watia Sahihi Mkataba wa Kuuza Majengo Kadhaa Huko Brooklyn

Mashahidi wa Yehova Watia Sahihi Mkataba wa Kuuza Majengo Kadhaa Huko Brooklyn

NEW YORK—Mnamo Julai 5, 2013, Mashahidi wa Yehova walitia sahihi mkataba wa kuuza eneo lenye majengo matano ambalo lilitumika hapo awali kwa ajili ya shughuli za uchapishaji huko Brooklyn, New York. Pia walitia sahihi mkataba wa kuuza jengo la makazi lenye ghorofa 30. Walifanya mkataba huo na Kampuni ya Kushner na ile ya RFR. Mashahidi wa Yehova wataanza kuhama majengo hayo matano Agosti mwaka huu. Watahama jengo la makazi la ghorofa 30 mwaka wa 2017.

David Semonian, msemaji wa Mashahidi wa Yehova anasema kwamba wanapovuka Daraja la Brooklyn wapita njia na wageni wanaotembelea jiji la New York City huona maandishi yaliyoandikwa kwenye majengo hayo yanayosema ‘Soma Neno la Mungu Biblia Kila Siku’ na ‘Soma Mnara wa Mlinzi na Amkeni!’ Msemaji huyo wa Mashahidi wa Yehova anaongezea kusema hivi: “Kwa miaka mingi, kazi zilizofanywa katika majengo haya zilieleza zaidi kuhusu historia ya tengenezo letu na umuhimu wetu wa kuwa hapa Brooklyn.” Kwa miaka 77, Mashahidi wa Yehova walitumia eneo hilo lenye majengo matano kuchapisha Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha nyingi. Majengo ya kwanza katika eneo hilo lenye majengo matano yalianza kutumiwa mnamo mwaka wa 1927, na kuanzia mwaka wa 1937, majengo mengine yaliongezwa. Wafanyakazi 1,000 hivi waliishi katika jengo la makazi la ghorofa 30 na wangeweza kwenda kufanya kazi katika eneo la uchapishaji bila kulazimika kusafiri nje ya mahali hapo.

Mashahidi wanauza majengo hayo kwa sababu wanahamia kaskazini mwa jiji la New York City. Hatua ya kwanza ya uhamaji huo ilianza mwaka wa 2004 wakati kazi ya kuchapa, kujalidi na kusafirisha machapisho nchini Marekani ilipohamishwa hadi Wallkill, New York. Kwa sasa, Mashahidi wa Yehova wamepanga kuhamisha makao yao makuu ya ulimwenguni pote hadi Warwick, New York, na ujenzi unakusudiwa kuanza mwishoni mwa mwaka huu.

Bwana Semonian anasema: “Tumefurahia kuwa Brooklyn kwa miaka mingi. Tumeyatumia majengo haya kuchapisha ujumbe wa Biblia unaowasaidia watu ulimwenguni pote. Kwa sasa tuna hamu ya kutumia makao yetu mapya huko Warwick kuendeleza kazi yetu ya kuwafundisha watu Biblia ulimwenguni pote.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1 718 560 5000