Hamia kwenye habari

APRILI 28, 2017
MAREKANI

Watu 400 Hivi Watembelea Makao Makuu ya Mashahidi wa Yehova Wakati wa Siku ya Wageni

Watu 400 Hivi Watembelea Makao Makuu ya Mashahidi wa Yehova Wakati wa Siku ya Wageni

NEW YORK—Jumamosi iliyopita, Mashahidi wa Yehova walikuwa na siku ya wageni katika makao makuu yaliyojengwa hivi karibuni katika eneo la Warwick, New York.Hiyo ilikuwa siku ya kwanza kati ya siku mbili za pekee za wageni. Troy Snyder, anayesimamia majengo ya makao makuu, anasema hivi: “Wageni 1,150 hivi wanakuja kutembelea makao yetu makuu kila juma. Lakini tulitaka kuwa na siku za wageni katika miisho juma hii miwili ili tuwashukuru majirani wetu ambao si Mashahidi na wengine waliotuunga mkono wakati wa ujenzi.”

Watu 395 walihudhuria siku ya wageni Jumamosi hii, nao walitia ndani majirani 205 pamoja na wafanyabiashara na wanakandarasi za ujenzi 190. Walipata viburudisho na walitembezwa katika eneo hilo kwa dakika 40. Matembezi hayo yalitia ndani video fupi iliyofuatwa na kipindi cha maswali na majibu.

Christopher Gow, mkaaji wa Tuxedo Park, New York, na mshiriki wa Kamati ya Kutoa Mashauri.

Christopher Gow, mkazi wa eneo lililo karibu la Tuxedo Park, alisema hivi: “Nilifurahi kukubali mwaliko wa kutembelea eneo hilo, nilitaka sana kuliona. Nilijua kwamba kulikuwa na mradi wa ujenzi, lakini ulifanywa kimya-kimya sana na kwa heshima hivi kwamba hukusikia chochote.”

Kwa kuwa Mashahidi walijenga makao yao makuu kando ya fuo za Ziwa Sterling Forest (Blue Lake), majirani wengi walisema kwamba walikuja hasa ili kuona jinsi mazingira yalivyoathiriwa na ujenzi huo.

Dakt. Richard Hull, profesa wa historia aliyestaafu wa Chuo Kikuu cha New York na mwanahistoria wa mji wa Warwick, New York.

Dakt. Richard Hull, profesa wa historia aliyestaafu wa Chuo Kikuu cha New York, anayeishi Warwick na ambaye ndiye mwanahistoria wa mji huo, anasema hivi: “Nimechunguza eneo hilo kwa miaka zaidi ya 50. Mashahidi wamejitahidi sana kupatanisha mahitaji yao na mazingira, hata kufikia kuzingatia mahitaji ya wanyama pori wa mbuga hiyo.”

Baada ya kutembelea eneo hilo, Bw. Gow, ambaye pia ni mshiriki wa Kamati ya Kutoa Mashauri ya Mbuga ya Tuxedo, alisema hivi: “Kila kitu ni cha kiwango cha juu, Mashahidi wamefanya kazi nzuri sana. Ujenzi wenu uliozingatia mazingira unatuchochea sana na ni mfano ambao sisi sote tunapaswa kuiga.”

Baada ya matembezi hayo, wageni walikaribishwa kuona maonyesho matatu yaliyo kwenye orofa juu na chini ya mapokezi. Maonyesho mawili yanaonyesha historia ya Mashahidi wa Yehova na kazi wanayofanya sasa ulimwenguni pote, na onyesho la tatu lina Biblia zisizopatikana kwa urahisi na vitu vya kale vinavyohusiana na Biblia.

Dakt. Hull alisema hivi: “Makao hayo hali ya juu sana. Ninaona kwamba walitafakari sana na kuona mahitaji ya wakati ujao kabla ya kuanza ujenzi. Sijatembelea chumba cha makumbusho, lakini ninatazamia kwa hamu kurudi.”

Bw. Snyder anasema hivi: “Tunahisi kwamba watu wanaoishi hapa walistahili pongezi ya pekee kwa kutuunga mkono na kutukaribisha kwa uchangamfu tangu tulipohamia eneo hili. Kwa hiyo, hizi siku mbili za wageni zimekusudiwa hususa kwa ajili ya majirani wetu ambao si Mashahidi.” Kwa wale waliopokea mwaliko au wanaishi hapa na hawakuweza kuhudhuria Jumamosi iliyopita, siku nyingine ya wageni imepangwa Jumamosi hii, Aprili 29, kuanzia saa 4:00 asubuhi hadi saa 10:00 jioni.

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

David A. Semonian, Ofisi ya Habari za Umma, +1-845-524-3000