Hamia kwenye habari

Zaidi ya wahubiri 42,000 walijitolea kufanya kazi ya kutoa msaada iliyoendelea kwa muda mrefu katika Amerika ya Kati.

APRILI 12, 2019
MEXICO

Mashahidi wa Yehova Wakamilisha Kazi ya Kutoa Msaada Baada ya Matetemeko ya Ardhi Kutokea Amerika ya Kati

Mashahidi wa Yehova Wakamilisha Kazi ya Kutoa Msaada Baada ya Matetemeko ya Ardhi Kutokea Amerika ya Kati

Mwaka 2017, Guatemala na Mexico zilikumbwa na matetemeko mawili makubwa ya ardhi. Mwezi Desemba 2018, ndugu zetu walikamilisha kazi kubwa ya kutoa msaada katika eneo hilo.

Ofisi ya tawi ya Amerika ya Kati ilianza kazi ya kutoa msaada kwa kuandaa mikutano kadhaa ya kuwatia moyo ndugu na dada walioathiriwa na janga hilo. Mikutano hiyo ilifanywa katika majimbo ya Chiapas, Morelos, Oaxaca, na Puebla, na hata katika jiji la Mexico City. Halmashauri 39 za Kutoa Msaada Wakati wa Msiba zilifanya kazi chini ya mwongozo wa Halmashauri ya Tawi ili kupanga kazi ya kujenga upya.

Mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Amerika ya Kati, Jesse Pérez, akizungumza na wahubiri walioathiriwa katika jimbo la Morelos.

Ndugu wawili wakirekebisha paa ya Jumba la Kusanyiko ambalo lilikuwa likijengwa upya wakati wa kazi ya kutoa msaada.

Zaidi ya wahubiri 42,000 wanaotoka majimbo tofauti-tofauti nchini Mexico walijitolea kushiriki katika kazi ya kutoa misaada. Walijenga upya nyumba 619, Majumba 5 ya Ufalme, na Majumba 2 ya Kusanyiko. Pia, walirekebisha nyumba nyingine 502 na Majumba 53 ya Ufalme. Nchini Guatemala, nyumba kumi zilijengwa upya.

Familia ya Hernández na ya Santiago ni baadhi ya Mashahidi waliopewa msaada.

Familia ya Hernández wakiwa wamesimama mbele ya nyumba yao ambayo ilijengwa upya na wajitoleaji.

Familia ya Hernández inaishi katika jiji la Chalco, umbali wa kilomita 40 kutoka jiji la Mexico City. Tetemeko la ardhi lililotokea Septemba 19, 2017, liliharibu nyumba yao kiasi cha kwamba haingeweza kurekebishwa. Dada Ana María Hernández anasema hivi: “Licha ya kupatwa na janga hilo, hatukuwahi kukosa chochote. Ndugu zetu walitutunza vizuri sana. Bado ninakumbuka kuwaona wajitoleaji 50 au zaidi wakiwa wamesimama mahali ambapo nyumba yetu ya awali ilikuwa na wakifanya kazi ili kuijenga upya. Mpaka leo hii, jirani zetu wanashangazwa na jambo ambalo akina ndugu walifanya.” Mbali na kutoa msaada wa kimwili, mwakilishi wa Halmashauri ya Tawi ya Amerika ya Kati alitembelea familia ya Hernández na kuwatia moyo kupitia Biblia.

Familia ya Santiago mbele ya nyumba yao mpya.

Familia ya Santiago, inayoishi kwenye mji wa Juchitán katika jimbo la Oaxaca, waliathiriwa na tetemeko la ardhi lililotokea Septemba 7, 2017. Nyumba yao iliharibika kiasi cha kwamba hawakuweza kuishi humo tena. Hata hivyo, wajitoleaji waliwajengea nyumba yao upya kwa kipindi kisichozidi miezi sita. Baba wa familia hiyo, Ndugu Victor Santiago, alisema hivi: “Nilistaajabishwa na jinsi ambavyo tengenezo la Yehova lilivyotoa msaada huo upesi. Nilimwona Yehova akiongoza mambo.”

Ndugu Jesse Pérez, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Amerika ya Kati, aliongezea hivi: “Matetemeko hayo mawili yalileta uharibifu mkubwa. Hata hivyo, kazi ya kutoa msaada iliyoendelea kwa muda mrefu iliwapatia ndugu na dada nafasi ya kuonyesha roho ya kujitolea. Wahubiri wengi walishiriki, na hivyo kuonyesha upendo wao wa kindugu. Tunafurahi kwamba Yehova alibariki ‘huduma hiyo ya kutoa msaada.’”—2 Wakorintho 8:1-4.