Hamia kwenye habari

Magari yaliyochomwa moto katika makabiliano huko Culiacán

NOVEMBA 8, 2019
MEXICO

Shahidi wa Yehova Auawa Katika Shambulizi la Kikatili Huko Culiacán, Mexico

Shahidi wa Yehova Auawa Katika Shambulizi la Kikatili Huko Culiacán, Mexico

Oktoba 17 ,2019, polisi na maofisa wa usalama nchini Mexico walikabiliana na kundi la wauza madawa ya kulevya waliokuwa na silaha zenye nguvu. Walishambuliana kwa risasi huko Culiacán, Sinaloa, nchini Mexico. Jiji la Culiacán lina wakaaji milioni moja hivi. Wakati wa makabiliano hayo, barabara kuu zilifungwa, magari yalichomwa moto, na wafungwa wakatoroka kutoka katika gereza lililo hapo karibu. Maofisa wanasema kwamba watu 14 hivi waliuawa. Kwa kusikitisha ofisi ya tawi ya Amerika ya Kati inaripoti kwamba mmoja wa ndugu zetu, Noé Beltrán, alikuwa kati ya wale waliouawa katika shambulizi hilo.

Noé Beltrán akiwa na watoto wake wawili

Ndugu Beltrán, mwenye umri wa miaka 39, baba ya watoto watatu, alikuwa kazini alipopigwa na risasi iliyorushwa kimakosa. Ndugu na dada wenyeji na mwangalizi wa mzunguko wanatumia maandiko kumfariji Rocío, mke wa ndugu Beltrán, pamoja na watoto wao.

Kuna zaidi ya wahubiri 7,000 katika makutaniko 80 huko Culiacán. Wakati wa mashambulizi hayo, kwa muda, baadhi ya makutaniko yalibadili mipango ya mikutano ya katikati ya juma na mikutano ya utumishi wa shambani. Baadhi ya ndugu na dada waliunganishwa na mikutano ya katikati ya juma wakiwa nyumbani. Waangalizi wa mizunguko wanaongoza kufanya ziara za uchungaji kwa wote waliopatwa na tukio hilo la kutisha ambalo halikutarajiwa.

Tunahuzunishwa sana na kifo cha Ndugu Beltrán, na tunasali kwamba Yehova aendelee kumtegemeza Dada Beltrán na watoto wake. Tunatazamia kwa hamu wakati ambapo dunia itakuwa na amani na badala ya huzuni kutakuwa na “shangwe kubwa sana.”—Marko 5:42.