Hamia kwenye habari

AGOSTI 19, 2021
MEXICO

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Yatolewa Katika Lugha ya Mixtec (Guerrero)

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Yatolewa Katika Lugha ya Mixtec (Guerrero)

Agosti 8, 2021, Ndugu José Nieto, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Amerika ya Kati, alitoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Mixtec (Guerrero). Biblia hiyo ilitolewa katika mfumo wa kielektroni wakati wa programu iliyorekodiwa mapema na kupeperushwa kwa watu 785. Ofisi ya tawi inatarajia kuchapisha nakala za Biblia hiyo kuanzia Novemba 2021 na kuzisafirisha kwa makutaniko mwezi Desemba 2021 au Januari 2022.

Wakati wa kutolewa kwa Biblia hiyo, Ndugu Nieto alisema hivi baada ya kusoma 1 Wakorintho 14:9: “Ili watu wafaidike kutokana na nguvu za Neno la Mungu, lazima Biblia ipatikane katika lugha ambayo kila mtu anaelewa . . . , lugha anayotumia kila siku.”

Mixtec (Guerrero) ni aina ya lugha ambayo sauti mbalimbali hutumiwa kutokeza maana tofauti za maneno. Inazungumzwa na watu 150,000 hivi katika jimbo la Guerrero, Mexico, na wengine wengi katika maeneo mengine ya Mexico na Marekani.

Ndugu Lázaro González, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Amerika ya Kati alisema hivi: “Watu wanaozungumza lugha ya Mixtec (Guerrero) wanaishi katika eneo lililokumbwa na umaskini na jeuri. Na sasa janga la COVID-19 limefanya hali iwe ngumu hata zaidi. Hilo limewafanya watu waamini kwamba Mungu amewaacha. Hata hivyo, kujipatia sehemu ya Biblia katika lugha yao ni uthibitisho wa wazi kwamba Yehova anawajali.”

Kabla ya kutolewa kwa Biblia hiyo, kulikuwa na tafsiri mbili tu za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Mixtec (Guerrero). Si rahisi kuelewa tafsiri hizo kwa sababu zilitokezwa na watu wa jamii mbili tofauti. Watafsiri hao walitumia maneno yanayoeleweka katika maeneo yao tu, na hilo lilifanya iwe vigumu kwa watu katika jamii nyingine kuelewa wanachosoma.

Mfano wa jinsi tafsiri hii mpya inavyoeleweka kwa urahisi ni maneno ya Mathayo 5:9 yanayosema: “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani.” Katika lugha ya Mixtec (Guerrero), hakuna neno hususa la “amani.” Ili kuwasilisha maana sahihi, mstari huo ulitafsiriwa hivi: “Wenye furaha ni watu wanaotafuta njia za kuzuia matatizo/usumbufu.” Hilo linapatana na maana ya neno la Kiingereza.

Mtafsiri mmoja alisema hivi: “Andiko moja ninalopenda sana ni 1 Petro 1:25, ambapo tunasoma kwamba ‘neno la Yehova linadumu milele.’ Siwezi kuwazia kuishi bila Biblia, nami ninamshukuru Yehova kwa kuilinda hadi leo. Na sasa, tuna Biblia katika lugha yetu wenyewe, Mixtec (Guerrero).”

Mtafsiri mmoja alisema hivi: “Sina shaka kwamba Yehova alituunga mkono kupitia roho yake takatifu. Nimesadiki kuliko wakati mwingine kwamba lugha haziwezi kumzuia Yehova. Ametuonyesha kwa mara nyingine kwamba Neno lake ‘halifungwi.’”—2 Timotheo 2:9.