Hamia kwenye habari

JULAI 23, 2021
MEXICO

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Yatolewa Katika Lugha ya Tojolabal

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Yatolewa Katika Lugha ya Tojolabal

Julai 18, 2021, Ndugu Arturo Manzanares, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Amerika ya Kati, alitangaza kutolewa kwa Tafsiri ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Tojolabal.

Lugha ya kienyeji ya Tojolabal inazungumzwa na zaidi ya watu 66,000, hasa katika eneo la Chiapas, Mexico, katika eneo la kusini-mashariki la nchi hiyo karibu na Guatemala. Biblia hiyo ilitolewa katika mfumo wa kielektroni wakati wa programu iliyopeperushwa kwa wasikilizaji 2,800 hivi.

Wakati wa programu hiyo, msemaji aliuliza hivi: “Kwa nini tunahitaji Biblia katika lugha ya Tojolabal?” Alijibu kwa kusema: “Kwa sababu ni muhimu kuwa na Biblia inayomletea sifa Mtungaji wake, Yehova.”

Dada aliyesaidia katika kazi ya kutafsiri alisema hivi: “Nilichochewa sana niliposoma Yohana 5:28, 29. Ningeweza kuwazia kihalisi kabisa mama yangu akifufuliwa. Nimesoma mistari hiyo mara nyingi katika Kihispania, lakini sasa ninaiposoma katika lugha yangu, ninaielewa kwa kina zaidi. Asanteni sana!”

Ofisi mpya ya utafsiri ya lugha ya Tojolabal iliyoko Las Margaritas, Chiapas

Wakati wa mradi huo, watafsiri wa lugha hiyo walihama kutoka ofisi ya tawi ya Amerika ya Kati, iliyo karibu na Mexico City, na kuhamia kwenye ofisi mpya ya utafsiri iliyoko Las Margaritas, Chiapas. Ofisi hiyo sasa iko katika eneo la watu wanaozungumza lugha ya Tojolabal, kilomita 990 kutoka kwenye ofisi ya tawi. Kwa sasa kuna watafsiri tisa wanaotumikia kwenye ofisi ya utafsiri, pamoja na ndugu watano wanaofanya kazi katika idara tegemezi. Ingawa watu wa jamii mbalimbali zinazozungumza lugha ya Tojolabal wanaweza kuelewana, kuna tofauti ndogo ya jinsi maneno fulani yanavyotumiwa. Watafsiri walikuwa makini sana kutafsiri Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika njia sahihi na inayoeleweka kwa urahisi na wengi.

Kwa mfano, Biblia za lugha hiyo hutafsiri “Ufalme wa Mungu” kuwa “mahali ambapo Mungu hutolea amri” au “mji (au jiji) wa Mungu.” Lakini wasomaji ambao hawatumii maneno hayo hawaelewi chochote wanapoyasoma. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Tojolabal inatumia maneno “Serikali ya Mungu,” na maneno hayo yanaeleweka waziwazi.

Dada mmoja aliyehudhuria programu hiyo alisema hivi: “Kwa kweli, Yehova aliwaongoza wote walioshiriki katika mradi huu ili waweze kutokeza tafsiri iliyo wazi, sahihi, na ambayo ni rahisi kusomeka. Nina uhakika kwamba zawadi hii itagusa mioyo ya watu wengi ambao bado hawamjui Mungu.”—Matendo 17:27.