Hamia kwenye habari

NOVEMBA 4, 2015
MEXICO

Mashahidi Wapata Tuzo kwa Kazi ya Elimu ya Biblia Kwenye Magereza ya Mexico

Mashahidi Wapata Tuzo kwa Kazi ya Elimu ya Biblia Kwenye Magereza ya Mexico

MEXICO CITY—Maofisa katika jimbo la Baja California, Mexico, wametoa cheti kwa ajili ya kuwashukuru Mashahidi wa Yehova kwa kazi ya elimu ya Biblia katika magereza ya jimboni hapo. Cheti hicho kilisainiwa na Daniel De La Rosa Anaya, katibu wa jimbo anayeshughulikia usalama wa jamii pamoja na Jesús Héctor Grijalva Tapia katibu wa jimbo anayeshughulikia magereza.

Cheti hicho kinasema hivi: “Serikali ya jimbo kupitia katibu wa usalama wa jamii ingependa kuwashukuru Mashahidi wa Yehova kwa msaada wao wenye thamani sana wa kujitolea kwa dhati kufanya kazi kwa ajili ya watu wa Baja California; kazi ambayo imeboresha maisha ya watu na kuwafanya wawe na tabia nzuri.”

Jesús Manuel López Moreno, Mkurugenzi wa Kituo cha Kurekebisha Tabia cha Mexicali.

Kila mara Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakitembelea magereza mbalimbali ya Baja California, kutia ndani gereza moja lililopo Mexicali, ambalo walianza kulitembelea mwaka 1991 baada ya kupokea maombi kutoka kwa wafungwa. Alipokuwa akihojiwa na Mashahidi, Jesús Manuel López Moreno, mkurugenzi wa kituo cha kurekebisha tabia cha Mexicali, alisema hivi: “Mnapokuja hapa na kuwahudumia [wafungwa] mnatusaidia kuwaimarisha ili wajitambue na kuhisi hivi: ‘Sisi ni wanadamu pia. Tuna thamani ileile na wakati ukifika tutatoka na kushirikiana vizuri na jamii ili kuleta maendeleo.’ . . . Ninawashukuru sana kwa msaada wenu.”

Gamaliel Camarillo, msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Mexico, alisema hivi: “Kazi ya msingi ya Mashahidi wa Yehova ni kuwasaidia watu, kutia ndani wafungwa, wafahamu yale ambayo Biblia inafundisha. Kutaniko la Mexicali limeripoti kwamba watu nane hivi walibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova walipokuwa wakitumikia vifungo vyao katika gereza la Mexicali. Tunaamini kwamba watu wa jamii zote wanapaswa kupata nafasi ya kunufaika na elimu ya Biblia.”

Wanahabari wanaweza kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya Habari za Umma, simu. +1 718 560 5000

Mexico: Gamaliel Camarillo, simu. +52 555 133 3048