Hamia kwenye habari

JUNI 7, 2017
MISRI

‘Ninatazamia Kuona Marufuku Isiyo ya Haki Ikiondolewa’

‘Ninatazamia Kuona Marufuku Isiyo ya Haki Ikiondolewa’

Ehab Samir mwenye umri wa miaka 52 ni raia wa Misri na Shahidi wa Yehova. Bw. Samir anasema kwamba kwa sababu ya vikwazo vingi vilivyowekwa na serikali ya Misri dhidi ya ibada yao, Mashahidi wengi wamekuwa wakitendewa na wenye mamlaka “kama wahalifu.” Makala iliyowekwa kwenye kituo fulani cha habari ilimfariji sana Bw. Samir kwa sababu ilitaja hali hizo kama zilivyo.

Makala hiyo ilikuwa na kichwa, “Dakt. Riham Atef Aandika: Mashahidi wa Yehova,” iliyochapishwa Agosti 19, 2016 na Shbab Misr, kituo cha habari za mtandaoni nchini Misri. Dakt. Atef, profesa msaidizi wa Chuo Kikuu cha Cairo na mwandishi wa habari, alielezea kwamba watu hawawaelewi Mashahidi nchini Misri. Yeye binafsi anafahamiana na baadhi ya Mashahidi wa Yehova na amefanya utafiti wa kutosha kuwahusu, alisema hivi: “Nimesadikishwa kwamba wanajali na kuheshimu imani za watu wengine.”

“Wanachochea Upendo na Amani”

Dakt. Atef anaeleza kwamba watu aliotarajia wasome makala hiyoni watu “ambao hawajui lolote kuhusu Mashahidi wa Yehova na ambao wanawachukia kwa sababu ya kutokuwa na habari sahihi kuwahusu.” Makala yake ilielezea kwa ufupi baadhi ya imani za msingi za Mashahidi na kueleza kwamba “kuna habari nyingi zinazopatikana katika tovuti yao ya www.pr418.com.”

Alipowachunguza Mashahidi wa Yehova bila ubaguzi, Dakt. Atef aliona tofauti kubwa kati ya mambo halisi na jinsi watu wanavyowaona Mashahidi wa Yehova nchini Misri. Alisema hivi: “Wamepigwa marufuku, na sielewi sababu. Wao hawaungi mkono upande wowote wa kisiasa. . . . Na wanachochea upendo na amani.” Dakt. Atef aliwaambia wasomaji hivi: “Je, hizo ndizo sababu za kuwapiga marufuku? Au wamepigwa marufuku kwa sababu mafundisho yao ya Biblia ni tofauti na mafundisho ya makanisa mengine?”

‘Ninatazamia Kuona Marufuku Ikiondolewa’

Bw Samir alifurahishwa sana na makala hiyo kuhusu Mashahidi hivi kwamba alichochewa kuandika barua ya kumshukuru mhariri. Alisema hivi: “Nimesoma makala nyingi katika vyombo vya habari [vya Misri] kuhusu Mashahidi wa Yehova, lakini makala chache sana zinatoa maelezo mazuri kuwahusu. Hivyo, ninampongeza Dakt. Riham Atef kwa ujasiri na unyoofu wake.” Kituo hicho cha habari za mtandaoni kilichapisha maelezo ya Bw. Samir Desemba 11, 2016.

Katika barua yake, Bw. Samir alieleza kwamba amevunjwa moyo na jinsi Mashahidi wanavyotendewa isivyo haki na alionyesha sababu ni habari za uwongo zinazotolewa na viongozi wa kanisa. Bw. Samir alieleza kwamba habari zisizo za kweli ni chanzo cha matendo yasiyo ya haki ambayo yeye binafsi amewahi kukabiliana nayo. Kisha akaeleza: “Njia bora ya kumjua mtu ni kuzungumza naye. Kwa hiyo ningependa kumshukuru Dakt. Riham Atef kwa mambo aliyoandika.”

Bw. Samir alimalizia barua yake kwa maelezo haya ya kutoka moyoni: “Ninatazamia kuona marufuku isiyo ya haki dhidi ya Mashahidi wa Yehova ikiondolewa ili tuweze kufanya ibada yetu kwa uhuru katika nchi yetu.”

Matarajio ya Uhuru wa Ibada

Miaka mingi iliyopita, Mashahidi wa Yehova walifurahia uhuru wa ibada nchini Misri na walikuwa wamesajiliwa kuwa dini inayotambulika. Hata hivyo, mwaka wa 1960, walipigwa marufuku na walikosa haki nyingi za kidini na za kibinadamu zinazotolewa kwa dini mbalimbali za Kikristo nchini Misri.

Tangu wakati huo, Mashahidi wa Yehova nchini Misri wameendelea kuthibitika kuwa watu wazuri katika jamii, “[wanaochochea] upendo na amani” katika kila hali, kama ilivyoelezwa na Dakt. Atef. Wengi wana tamaa kama ya Bw. Samir kuona Mashahidi wakipata haki zao za msingi na kufurahia tena uhuru wa ibada nchini Misri.