Hamia kwenye habari

JUNI 22, 2023
MSUMBIJI

Biblia Nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Yatolewa Katika Kichangana (cha Msumbiji)

Biblia Nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Yatolewa Katika Kichangana (cha Msumbiji)

Juni 18, 2023, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa ikiwa nzima katika Kichangana (cha Msumbiji). Ndugu Charles Fonseca, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Msumbiji, alitangaza kutolewa kwa Biblia hiyo katika programu iliyohudhuriwa na watu 16,245. Programu hiyo ilifanyiwa Maputo, mji mkuu wa Msumbiji. Wale waliohudhuria walipata nakala zilizochapishwa. Isitoshe, nakala za kielektroni zilipatikana kwa ajili ya kupakuliwa.

Kichangana (cha Msumbiji) kinazungumzwa na watu milioni 4.2 hivi. Wengi kati ya watu hao, wanapatikana hasa katika mikoa miwili iliyo kusini mwa Msumbiji, yaani, mkoa wa Maputo na Gaza. Kwa kuwa Kichangana (cha Msumbiji) kina lahaja nyingi, watafsiri walijitahidi kutafuta na kutumia maneno ambayo watu wengi wanaozungumza Kichangana (cha Msumbiji) wanaelewa, hata iwe wanaishi wapi.

Kabla ya kupata Biblia nzima katika lugha yao, wahubiri wengi wanaozungumza Kichangana (cha Msumbiji) walitumia Biblia ya Kitsonga, lugha inayokaribiana na Kichangana (cha Msumbiji). Kwa sababu hiyo, ilikuwa vigumu kwa wengine kujifunza kweli za Biblia. Mtafsiri mmoja alisema: “Kwa kuwa sasa tuna tafsiri hii mpya, ujumbe wa Biblia unaweza kugusa kabisa mioyo ya wale wanaozungumza Kichangana (cha Msumbiji).”

Mtafsiri mwingine alitoa mfano ulioonyesha jinsi Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kichangana (cha Msumbiji) ilivyo wazi zaidi. Alisema: “Baadhi ya tafsiri za Biblia za lugha zinazozungumzwa katika eneo hili zimetafsiri neno ‘roho’ kwa maneno ambayo yanaweza kueleweka vibaya na kutokeza maana kwamba roho ni kiumbe kinachoendelea kuishi baada ya mwili kufa. Hata hivyo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kichangana (cha Msumbiji) inawasilisha maana sahihi kwa sababu inaonyesha kwamba ‘nguvu za uhai’ ndizo humrudia Muumba, na si mtu mwenyewe anayemrudia Muumba.”

Tunashangilia tunapoona jinsi Yehova ‘anavyoituma nuru yake na kweli yake’ kwa sababu watu wanaozungumza Kichangana (cha Msumbiji) wanaendelea kulielewa vizuri zaidi Neno lake.​— Zaburi 43:3.