Hamia kwenye habari

Ndugu Amaro Teixeira akitoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Ndau

MACHI 2, 2021
MSUMBIJI

Mashahidi wa Yehova Wafikia Hatua Muhimu Katika Kazi ya Kutafsiri Baada ya Kutolewa kwa Biblia Nchini Msumbiji

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Sasa Inapatikana Katika Lugha 200

Mashahidi wa Yehova Wafikia Hatua Muhimu Katika Kazi ya Kutafsiri Baada ya Kutolewa kwa Biblia Nchini Msumbiji

Februari 28, 2021 Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa katika lugha ya Ndau. Sasa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana katika lugha 200 ikiwa nzima au sehemu. Isitoshe, siku moja tu kabla ya hapo, Februari 27, Biblia—Injili Kulingana na Mathayo ilitolewa katika lugha ya Chuabo.

Ndugu Amaro Teixeira, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Msumbiji, alitoa tafsiri zote mbili katika mfumo wa kielektroni wakati wa programu zilizorekodiwa mapema na kurushwa kwa wahubiri. Isitoshe, programu hizo zilipeperushwa kwenye kituo cha televisheni cha kitaifa na vituo kadhaa vya redio. Biblia—Injili Kulingana na Mathayo iliyotolewa katika lugha ya Chuabo itapatikana pia katika broshua yenye kurasa 64 kwa ajili ya wale ambao hawawezi kutumia vifaa vya kielektroni.

Kichuabo ni lugha inayozungumzwa na watu milioni 1.4 katika Jimbo la Zambezia. Kuna wahubiri 492 katika makutaniko ya Kichuabo.

Ndugu Nicholas Ahladis, anayefanya katika idara ya Huduma za Tafsiri kwenye makao makuu, anasema hivi: “Tafsiri ya kitabu cha Mathayo katika lugha ya Chuabo ni hatua muhimu. Haikuwa rahisi kupata wala kuelewa tafsiri ya awali.”

Ndau ni lugha inayozungumzwa na watu milioni 1.1 hivi katikati mwa Msumbiji. Kuna wahubiri 1,500 wanaozungumza lugha hiyo.

Wakati wa mradi huo, kazi ya kutafsiri Kindau iliathiriwa na majanga matatu makubwa. Mnamo 2019, Kimbunga Idai kilisababisha uharibifu mkubwa nchini Msumbiji. Mwaka uliofuata, Msumbiji ilikumbwa na hali ngumu zilizotokana na ugonjwa wa virusi vya corona (COVID-19) kama tu sehemu nyingine ulimwenguni. Kisha, mapema mwaka wa 2021, Kimbunga Eloise kilisababisha uharibifu mkubwa nchini humo. Licha ya hali hizo ngumu, kikundi cha watafsiri watano kilikamilisha kazi yao katika muda wa miaka miwili na nusu.

Mshiriki mmoja wa kikundi cha utafsiri cha lugha ya Ndau anaeleza hivi: “Ninapoona matokeo, licha ya changamoto zote, bado siwezi kuamini kwamba tulifaulu kumaliza kazi hii. Kwa maoni yangu, huu ni muujiza. Mradi huu ulionekana unazidi uwezo na hali zetu, na matokeo yamepita tulichotarajia. Sifa zote zinamwendea Yehova.”

Ndugu Ahladis anaendelea kusema: “Ndugu zetu wanaozungumza lugha ya Ndau, kutia ndani watafsiri, wamepatwa na majaribu mengi katika nyakati za karibuni, ambayo yalichelewesha mradi wa kutafsiri Biblia hiyo. Lakini sasa, toleo hili la Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo linaloweza kueleweka kwa urahisi ni thawabu kubwa kwa ndugu zetu na litawatia moyo na kuwafariji watu wote wanaozungumza lugha ya Ndau.”

Ndugu Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza la Wazee, anasema: “Kila mradi wa kutafsiri Biblia unahusisha kujidhabihu na una changamoto. Baada ya hali ngumu ambazo kikundi cha utafsiri cha lugha ya Ndau, kutia ndani misiba ya asili, inafaa sana kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Ndau kutolewa ikiwa lugha namba 200. Tuna uhakika kwamba Biblia hii itakuwa baraka kubwa kwa watu wanaozungumza Kindau nchini Msumbiji.”

Tunashangilia pamoja na ndugu zetu baada ya kutolewa kwa Biblia hizo huku ugonjwa wa corona ukiendelea. Ni wazi kwamba hakuna kitu kinachoweza kumzuia Yehova kutimiza mapenzi yake.—Isaya 43:13.