Hamia kwenye habari

JUNI 17, 2015
NEPAL

Mashahidi wa Yehova Kutoka Nchi Mbalimbali Wanasaidia Waathiriwa wa Tetemeko la Ardhi Nchini Nepal

Mashahidi wa Yehova Kutoka Nchi Mbalimbali Wanasaidia Waathiriwa wa Tetemeko la Ardhi Nchini Nepal

KATHMANDU, Nepal—Mashahidi wa Yehova kutoka Bangladesh, Ujerumani, India, Japani, Uswisi, na Marekani wanaendelea kuwasaidia waathiriwa wa tetemeko kubwa la ardhi lililoipiga Nepal mnamo Aprili 25, 2015, na kuua maelfu ya watu, kutia ndani Shahidi mmoja wa Yehova na watoto wake wawili. Tetemeko la pili lilipiga Nepal mnamo Mei 12, 2015. Mashahidi wamesema kwamba katika tetemeko hilo la pili hakuna washiriki wao wowote waliojeruhiwa sana, mali zao kuharibiwa, au kupoteza maisha.

Mashahidi wa Yehova walitoa msaada wa chakula kwa waabudu wenzao na waathirika wengine wa tetemeko mara mbili kwa siku.

Siku moja baada ya tetemeko la kwanza kutokea, wawakilishi kutoka ofisi ya Mashahidi wa Yehova ya Nepal walitembelea kila kutaniko ili kujua mahitaji ya waathirika katika eneo la Bonde la Kathmandu, eneo lililoathiriwa sana na tetemeko. Tetemeko hilo liliharibu kabisa nyumba 38 za Mashahidi na nyingine 126 hazikuharibika sana. Mashahidi hao waliokosa makao walikaribishwa na kuishi kwa muda katika nyumba za waabudu wenzao, nyumba za ibada zinazoitwa Majumba ya Ufalme, na mahema yaliyowekwa katika maeneo yaliyokuwa wazi. Ofisi ya Nepal ilianza kutoa msaada wa chakula na baada ya muda misaada zaidi kutoka Bangladesh, India na majiji ya yaliyopo nchini Nepal ya Birgunj, Damauli, Mahendranagar, na Pokhara. Halmashauri ya Kutoa Msaada inasimamia kazi ya kujenga makazi ya muda inayofanywa na Mashahidi wajitoleaji kutoka India, Japani, na Nepal.

Wajitoleaji kutoka ofisi ya Mashahidi wa Yehova nchini Nepal wakihifadhi misaada iliyofika kutoka jiji la Birgunj, nchini Nepal.

Msemaji wa Mashahidi wa Yehova nchini Nepal, Reuben Thapaliya, anasema hivi: “Mbali na kuwapa msaada wa kimwili waathiriwa wa tetemeko, tunajitahidi pia kuwapatia msaada wa kiroho. Tunawapa chakula, maji, makazi na msaada wa kiroho.” Kuanzia Mei 2-5, 2015, Gary Breaux, mwakilishi kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova, alitembelea makutaniko na familia moja-moja zilizoathiriwa na tetemeko hilo. Mei 4, 2015, Bwana Breaux alitoa hotuba iliyotegemea Biblia katika programu ya pekee iliyounganishwa kwa njia ya video kwa makutaniko ya eneo hilo. Pia, Mei 5, 2015, Kenji Chichii, mwakilishi kutoka ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Japani aliwasili Nepal. Yeye pia alitembelea familia zilizoathiriwa na tetemeko hilo na akatoa hotuba zenye kutia moyo zilizotegemea Biblia.

Gary Breaux (kulia), mwakilishi kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova akikagua nyumba iliyoharibiwa na tetemeko la ardhi

Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani iliunda timu ya madaktari Mashahidi iliyokuwa na muuguzi, mtaalamu wa unusukaputi, upasuaji, na mhudumu wa matibabu ya dharura. Wakiwa na dawa zilizotolewa na Mashahidi kutoka Bangladesh, India, na Japani, na vifaa vingine vya kufanyia upasuaji na kushughulikia wagonjwa mahututi, timu hiyo kutoka Ulaya ilishirikiana na Halmashauri ya Kutoa Msaada ya Nepal kutoa huduma ya tiba kwa wagonjwa katika Majumba ya Ufalme yaliyopo katika eneo lilikumbwa na tetemeko la ardhi.

Timu ya kutoa msaada ikiwa katika Jumba la Ufalme jijini Kathmandu ambapo Mashahidi walioathirika na tetemeko la ardhi wanapewa chakula na makazi.

J. R. Brown, msemaji katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova, anasema hivi: “Bado tunaendelea kutoa msaada kwa kuwa tunatambua kwamba kwa kawaida waathirika wa janga lolote wana mahitaji mengi zaidi ya kupona kimwili. Tungependa kuwahakikishia waabudu wenzetu nchini Nepal na wote waliokoka tetemeko hilo la ardhi kwamba tutaendelea kuwapatia msaada wa kiroho na kimwili. Tunawakumbuka na tunasali kwa ajili yao.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

J. R. Brown, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1 718 560 5000

Ujerumani: Wolfram Slupina, simu +49 6483 41 3110

Japani: Ichiki Matsunaga, simu +81 46 233 0005

Nepal: Reuben Thapaliya, simu +977 9813469616