Hamia kwenye habari

SEPTEMBA 2, 2019
RWANDA

Mashahidi wa Yehova Wafanya Kusanyiko la Kwanza la Eneo Katika Lugha ya Ishara ya Rwanda

Mashahidi wa Yehova Wafanya Kusanyiko la Kwanza la Eneo Katika Lugha ya Ishara ya Rwanda

Kuanzia Agosti 16 hadi 18, 2019, ndugu zetu walifanya kusanyiko la kwanza la eneo katika Lugha ya Ishara ya Rwanda (RWS) huko Kigali, Rwanda. Hudhurio lilikuwa watu 620, na viziwi 8 walibatizwa.

Wahudhuriaji wakiimba wimbo wa Ufalme katika lugha ya Ishara

Maofisa wawili wa umma walihudhuria kusanyiko siku ya Jumapili: Bw. Jean Damascène Bizimana, aliye kwenye halmashauri ya wakurugenzi ya Muungano wa Kitaifa wa Viziwi Nchini Rwanda, na Bw. Emmanuel Ndayisaba, katibu mkuu wa Baraza la Kitaifa la Watu Wenye Ulemavu. Isitoshe, gazeti la Ukwezi liliripoti kwa njia nzuri kuhusu programu ya kusanyiko siku ya Jumapili na kuchapisha habari hizo mtandaoni.

Dada akimtafsiria programu ya kusanyiko mtu ambaye ni kipofu na kiziwi kwa kutumia mikono

Bw. Bizimana alisema: “Hili lilikuwa kusanyiko bora! Kuwaona viziwi kutoka maeneo mbalimbali ya nchi wakiwa wamekusanyika—asanteni sana. Tunawashukuru sana Mashahidi wa Yehova kwa kuunga mkono mawasiliano ya viziwi. Maofisa wa serikali wanapaswa kuhudhuria tukio kama hili lenye kuleta umoja na kuliiga.”

Kwa kipindi cha miaka miwili iliyopita, kumekuwa na hatua mbili kubwa katika Lugha ya Ishara ya Rwanda. Mnamo Septemba 2017, ofisi ya tawi ya Rwanda ilifanya shule ya kwanza ya mapainia katika Lugha ya Ishara ya Rwanda. Mwaka mmoja baadaye, mnamo Septemba 2018, ofisi ya tawi ilianza rasmi kutafsiri machapisho yetu katika Lugha ya Ishara ya Rwanda.

Ndugu Jean d’Amour Habiyaremye, aliyekuwa mwakilishi wa ofisi ya tawi kwenye kusanyiko hilo la lugha ya ishara, alisema: “Tunafurahi sana kuona maendeleo katika Lugha ya Ishara ya Rwanda, kutia ndani kusanyiko hili la eneo. Kichwa cha programu, ‘Upendo Haushindwi Kamwe!’ kinaonekana wazi kupitia jinsi ambavyo Mashahidi wa Yehova wanawaonyesha watu upendo, kutia ndani viziwi.”

Maendeleo katika lugha ya ishara ni uthibitisho ulio wazi kwamba Yehova anaendelea kutubariki sana!—Zaburi 67:1.