Hamia kwenye habari

Familia nchini Sierra Leone ikiwa na nakala mpya za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Krio, muda mfupi baada ya hotuba ya kutolewa kwenye kituo cha taifa cha televisheni

MEI 4, 2020
SIERRA LEONE

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Sasa Inapatikana Katika Kikrio

Imetolewa Nchini Sierra Leone Kwenye Redio na Televisheni ya Taifa

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Sasa Inapatikana Katika Kikrio

Aprili 26, 2020, zaidi ya wahubiri 2,000 wanaozungumza Kikrio nchini Sierra Leone walifurahi Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilipotolewa.

Haikuwezekana kwa ndugu zetu kukutana kwa ajili ya tukio hilo la pekee, kwa kuwa mwongozo wa serikali kuhusiana na ugonjwa wa virusi vya corona ulizuia vikusanyiko. Isitoshe, akina ndugu hawangeweza kuunganisha tukio hilo la pekee kupitia Intaneti kwa kuwa wahubiri wengi nchini Sierra Leone, hasa walio katika majiji madogo, hawana vifaa vya kielektroni.

Ndugu Alfred Gunn, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Liberia, akitoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kikrio

Kwa sababu hiyo, Halmashauri ya Tawi ya Liberia, ambayo inasimamia kazi nchini Sierra Leone, ilipata kibali kutoka kwa Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza ya kurekodi programu iliyofupishwa ya programu ya kutolewa kwa Biblia hiyo. Wahubiri walielekezwa wasikilize programu hiyo kwenye redio au televisheni, lakini hawakujulishwa kwamba Biblia ingetolewa.

Siku chache kabla ya kutolewa kwa Biblia hiyo, bahasha zilizofungwa zilizokuwa na Biblia hizo mpya zilipelekwa kwenye nyumba za wahubiri. Bahasha hizo zilikuwa na maagizo kwamba hawapaswi kuzifungua hadi baada ya programu hiyo ya pekee.

Mara tu baada ya Biblia hiyo kutolewa, Dada Megan Diaz, aliyehamia nchini Sierra Leone ili kutumikia eneo lenye uhitaji mkubwa, alisema hivi: “Mwanafunzi wangu wa Biblia alinipigia simu kwamba alisikiliza hotuba hiyo na kwamba anafurahi sana Yehova alifanya tupate tafsiri hiyo! Tutatumia tafsiri yetu mpya wakati wa funzo.”

Tounkara ni mwanafunzi wa Biblia anayezungumza Kikrio. Alisema hivi: “Kutolewa kwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kikrio ni uthibitisho wenye kusadikisha kwamba Yehova anataka ujumbe wake uwafikie watu wote, si ili tu wajifunze bali pia wauelewe vizuri sana kiasi cha kuwafundisha watoto wao. Ninafurahi sana kupata tafsiri hii mpya katika lugha yetu.”

Lugha ya Krio inatokana na Kiingereza na ndiyo lugha inayozungumzwa na watu wengi zaidi nchini Sierra Leone. Watafsiri wanne walitumia miaka miwili na nusu kutafsiri Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kikrio. Toleo la kielektroni liliwekwa kwenye jw.org Jumatatu, Aprili 27 ili liweze kupakuliwa.

Tukiwa pamoja na ndugu na dada nchini Sierra Leone, tunamshukuru sana Yehova kwa toleo jipya la Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kikrio. Hii ni ‘zawadi njema na tuzo kamilifu’ kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni, Yehova.—Yakobo 1:17.