Hamia kwenye habari

OKTOBA 13, 2022
TAJIKISTAN

Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Kibinadamu Yatangaza Marufuku Dhidi ya Mashahidi wa Yehova Nchini Tajikistan ni Kinyume cha Sheria

Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Kibinadamu Yatangaza Marufuku Dhidi ya Mashahidi wa Yehova Nchini Tajikistan ni Kinyume cha Sheria

Septemba 7, 2022, Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Kibinadamu (CCPR) ilitangaza uamuzi muhimu dhidi ya serikali ya Tajikistan kwa sababu iliwatendea Mashahidi wa Yehova kwa njia isiyo ya haki. Katika uamuzi uliofanywa Julai 7, 2022, wa kesi inayomhusu Adyrkhayev v. Tajikistan, CCPR iliwaunga mkono Mashahidi wa Yehova. Katika kesi hiyo, serikali ya Tajikistan ilishtakiwa kwa kukataa kuwasajili kisheria Mashahidi wa Yehova na kupiga marufuku utendaji wao.

Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakifanya ibada yao nchini Tajikistan kwa zaidi ya miaka 50. Shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova linaloitwa Religious Association of Jehovah’s Witnesses (RAJW) lilisajiliwa mwaka wa 1994. Hata hivyo, Wizara ya Utamaduni, ilifutilia mbali usajili huo na kupiga marufuku ibada ya Mashahidi wa Yehova. Serikali ilidai kwamba kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova, kukataa kwao kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri, na kuamini kwamba dini yao tu ndio ya kweli, ni kuwa na msimamo mkali. Jitihada ambazo Mashahidi wa Yehova wamefanya ili kusajili tena Shirika la RAJW zimegonga mwamba.

Katika uamuzi ambao CCPR ilifanya hivi karibuni, iliamua kwamba Tajikistan ilitenda kinyume cha sheria ilipowapiga marufuku Mashahidi wa Yehova. Ilisema kwamba “hakuna sababu yoyote kati ya zile zilizotolewa” na Tajikistan zinazohalalisha uamuzi wao wa kupiga marufuku Shirika la RAJW na kukataa kuwasajili tena.

CCPR pia ilisema kwamba baada ya serikali ya Tajikistan kukataa kusajili tena shirika la RAJW, Mashahidi wa Yehova “walikamatwa, waliwekwa mahabusu, walihojiwa, nyumba zao zilifanyiwa msako, walipigwa, machapisho yao ya kidini yalichukuliwa, na hata Shahidi mmoja wa Yehova alifukuzwa nchini humo.” Kwa sababu ya matendo hayo ya uonevu, CCPR iliamua kwamba haki za Mashahidi wa Yehova chini ya Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa wa Umoja wa Mataifa, zilikuwa zimekiukwa.

Ndugu Shamil Khakimov mwenye umri wa miaka sabini na moja amefungwa gerezani tangu Februari 2019

CCPR, iliiagiza serikali ya Tajikistan kukubali ombi la Mashahidi wa Yehova la kuwasajili kisheria, na kuwalipa fidia wale ambao haki zao zimekiukwa. Pia, serikali ya Tajikistan iliambiwa kwamba iko “chini ya wajibu wa kuchukua hatua zote zinazohitajika ili kuhakikisha kwamba ukiukaji wa sheria kama huo hautokei tena.”

Huenda uamuzi huo wa CCPR, ukawa na matokeo mazuri katika kesi ya Ndugu Shamil Khakimov, mwenye umri wa miaka 71, ambaye amefungwa gerezani tangu Februari 2019 kwa sababu ya kushiriki utendaji wa kidini kwa amani. Sababu ya pekee ambayo mamlaka ya Tajikistan imetumia ili kumkamata na kumfunga ndugu huyo ni marufuku dhidi ya Mashahidi wa Yehova.

Ni matumaini yetu kwamba, uamuzi wa CCPR, utafungua njia ya uhuru wa ibada kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova nchini Tajikistan. Tunasali kwamba Yehova aendelee kubariki jitihada zetu za “kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema.”​—Wafilipi 1:7.